Waziri wa mambo ya nje wa Sudan Mohamed Ali Ahmed Karti amewasili mjini Cairo kujiunga na wenzake wa Misri na Ethiopia kwa mjadala wa nchi hizo tatu kuhusu swala tata la bwawa linalojengwa na Ethiopia na njia za kuimarisha ushirikiano kati ya nchi hizo tatu zinazotegemea zaidi Mto Nile.
Nchi tatu hizo zilisaini kanuni juu ya Bwawa hilo wakati wa mkutano wao mjini Khartoum mwezi Machi.
Hata hivyo, tangu wakati huo, mjadala mkali umekuwa ukiendelea kuhusu taratibu na kanuni za msingi zilizotiwa saini.
Misri inahofu kwamba bwawa hilo litakupunguza sehemu yake ya maji ya mto Nile lakini Ethiopia imesema mradi huo hautakuwa na athari kwa Sudan na Misri katika mto huo.
Asilimia 30 ya ujenzi wa bwawa hilo linalokalia eneo la kilomita za mraba 1,800 umekamilika kwa sasa, na mradi mzima umepangwa kukamilika katika kipindi cha miaka mitatu kwa gharama ya dola bilioni 4.7 za kimarekani.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |