Baada ya kuruka kwa siku mbili, chombo cha kusafirisha mizigo cha Dragon CRS9 kilichorushwa na kampuni ya SpaceX ya Marekani tarehe 20 kilifika kituo cha anga ya juu cha kimataifa.
Saa 12 na dakika 56 asubuhi kwa saa za mashariki mwa Marekani, wanaanga wa Marekani Jeff Williams na Kathleen Rubins walioko katika kituo cha anga ya juu wakiendesha mikono mikubwa ya mashine ya kituo hiki, walishika chombo cha Dragon CRS9.
Hii ni mara ya 9 kwa chombo hiki kusafirisha mizigo kwenda kituo cha anga ya juu. Mara hii kimepeleka kifaa kipya cha kuunganisha vyombo vya safari ya anga ya juu, ambacho kitatumiwa kupokea vyombo vinavyobeba binadamu vitakavyorushwa na makampuni mbalimbali yakiwemo SpaceX na Boeing katika siku zijazo.
Chombo hiki pia kimepeleka kifaa cha kwanza cha kupima DNA katika anga ya juu, ambacho ukubwa wake ni sawa na simu ya mkononi na kitatumiwa kupima sampuli za DNA za virusi, vijidudu na panya. Kifaa kingine kilichopelekwa huko kitatumiwa kutafiti mabadiliko ya mioyo ya binadamu katika mazingira yenye mvutano mdogo wa dunia, na tofauti ya mabadiliko hayo kati ya watu mbalimbali.
Chombo hiki kilirushwa angani tarehe 18 na roketi ya Falcon 9 huko Florida, na kitakaa katika kituo cha anga ya juu mpaka tarehe 29 Agosti.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |