Chombo cha anga za juu kinachobeba wanaanga cha Shenzhou-11 kinatarajiwa kurushwa saa moja na nusu kesho asubuhi kwa saa za Beijing.
Akiongea na wanahabari leo kwenye kituo cha kurusha satelaiti cha Jiuquan, naibu mkurugenzi wa ofisi ya uhandisi wa chombo cha anga za juu kinachobeba wanaanga Wu Ping amesema chombo hicho kitabeba wanaanga wawili wanaume, Jing Haipeng na Chen Dong. Amesema chombo hicho kitakachorushwa kwa roketi aina ya Long March 2F kitaungana na maabara ya anga za juu ya Tiangong-2 ndani ya siku mbili, na wanaanga watakaa kwenye maabara hiyo kwa siku 30.
Amesema baada ya hapo chombo cha Shenzhou-11 kitatengana na Tiangong-2 na kurejea duniani ndani ya siku moja. Kazi hiyo inalenga kupeleka wanaanga na vifaa kwenye maabara ya Tiangong-2, na kutathmini teknolojia za vyombo vya anga za juu za kukutana, kuungana na kurudi duniani.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |