Ili kupambana na tishio kubwa la UKIMWI, serikali ya Afrika Kusini na pande zote za jamii zimeanzisha vita dhidi ya UKIMWI. Hivi sasa, Afrika Kusini imepata mafanikio makubwa yanayosifiwa duniani katika kupambana na UKIMWI.
Nchini Afrika Kusini, idadi ya maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto wakati wa kujifungua imepungua na kufikia asilimia 1.5 kutoka asilimia 30 ya miaka kumi iliyopita. Waziri wa afya wa Afrika Kusini Bw. Pakishe Motsoaledi amesema katika miaka mitano ijayo, Afrika Kusini itafanya juhudi zote za kupunguza asilimia hiyo hadi kufikia 0.8, na hatimaye kuiondoa kabisa.
Bibi Anna mwenye umri wa miaka 33 ni mmoja wa watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI nchini Afrika Kusini, amesema aligunduliwa kuwa ana virusi vya UKIMWI mwaka 2006, na amenufaika na mradi wa serikali wa kupambana na UKIMWI na kupata maisha bora. Amejifungua watoto wawili wenye afya nzuri. Yeye amekuwa mtu anayejitolea katika kuwaelimisha wengine kuhusiana na UKIMWI.
Serikali ya Afrika Kusini inatenga zaidi ya dola bilioni moja za kimarekani kila mwaka ili kupambana na UKIMWI, hasa katika kuwapatia wagonjwa wa UKIMWI matibabu ya dawa za Anti-Retroviral. Kuanzia mwaka 2010, idadi ya watu wanaokufa kutokana na UKIMWI nchini Afrika Kusini imepungua sana.
Hivi sasa, watu wengi zaidi wa Afrika Kusini wanafahamu umuhimu wa kujikinga dhidi ya UKIMWI. Serikali ya Afrika Kusini inatoa wito kwa wananchi wote wajiunge na harakati za kupambana na UKIMWI na kufanyiwa upimaji kwa hiari. Tangu mwaka 2010, watu milioni 30 wa Afrika Kusini wamepimwa. Lengo la serikali ya Afrika Kusini ni kuhakikisha kwamba kila mwaka kila mwananchi anapimwa walau mara moja, ili watu wanaoshi na virusi vya UKIMWI waweze kupata matibabu haraka iwezekanavyo. Zaidi ya hayo, Afrika Kusini imetunga sheria husika ili kulinda haki za watu walioiambukizwa virusi vya UKIMWI na wale wenye hatari ya kuambukizwa kirahisi.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |