Ofisi ya uchunguzi wa ndani ya Umoja wa mataifa imemaliza uchunguzi kuhusu tuhuma za udhalilishaji wa kijinsia dhidi ya walinzi wa amani wa umoja huo kutoka Gabon na Burundi, unaodaiwa kufanywa katika wilaya ya Kemo nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Msemaji wa Umoja wa mataifa Bw Stephane Dujarric amesema walinda amani hao wanatuhumiwa kufanya uhalifu huo kati ya mwaka 2014 na 2015. Wahanga 139 walihojiwa na kuwatambulisha kwa njia ya picha na kwa ushahidi mwingine, wahusika 16 kutoka Gabon, na wengine 25 kutoka Burundi.
Umoja wa mataifa umewasilisha ushahidi huo kwa serikali za Burundi na Gabon, na kutaka wahusika wachukuliwe hatua za kisheria.
Ripoti ya Umoja wa mataifa inasema jumla ya matukio 99 ya udhalilishaji wa kijinsia dhidi ya walinzi wa amani wa Umoja wa mataifa yaliripotiwa mwaka jana.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |