Mabingwa wa ligi kuu Tanzania Yanga SC wanatarajia kushuka dimbani leo kutupa kete yao ya pili kwenye michuano ya Sportpesa Super Cup dhidi ya AFC Leopards ya Kenya huku macho ya watanzania yakiwa kwa timu hiyo kuona kama itaweza kuleta ubingwa.
Timu ya Yanga ndiyo timu pekee inayoiwakilisha Tanzania katika mashindano hayo baada ya Mabingwa wa Kombe la Shirikisho Simba SC, Singida United na Jang'ombe ya Zanzibar kutolewa mapema katika hatua ya robo fainali ya michuano yenye mvuto wa aina yake.
Aidha leo kutakuwa na mechi nyingine tofauti na Yanga ambayo itawakutanisha Gor Mahia dhidi ya Nakuru All Stars zote kutoka Kenya katika hatua ya nusu fainali.
Katika mechi za leo timu itakayofanikiwa kumfunga mwenzake basi itakuwa imejikatia tiketi ya moja kwa moja kuingia katika fainali ya michuano ya Sportpesa Super Cup 2017 kuwania kitita cha Dola za kimarekani 30,000.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |