Kiongozi wa muungano wa vyama vya upinzani nchini Kenya NASA Raila Odinga ameanzisha kampeni ya kuleta mabadiliko katika tume ya uchaguzi na mipaka ya Kenya IEBC kabla ya kushiriki tena kwenye uchaguzi wa Oktoba 17.
Akiongea na wanahabari Bw. Odinga amesema uchaguzi utakaorudiwa hautakuwa wa haki, huru na wa kuaminika kama utaandaliwa na maofisa wa IEBC waliopo sasa ambao walisababisha wizi wa kura kwenye uchaguzi wa Agosti 8. Amesisitiza kuwa watazunguka nchi nzima kuwaelezea waungaji mkono wao kwanini tume ya sasa haiwezi kuaminika kuendesha uchaguzi huru na wa haki.
Bw. Odinga pia ameishutumu serikali kwa kushirikiana na tume hiyo kufanya vitendo viovu, akisema IEBC lazima ifanyiwe mabadiliko kupitia mchakato wa mashauriano kabla ya kufanyika kwa uchaguzi. Na ameapa kwamba hatapumzika hadi makamishna na maofisa 9 wa ngazi ya juu wa tume hiyo wajiuzulu kabla ya uchaguzi wa mwezi ujao.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |