Somalia na Tume ya kulinda amani ya Umoja wa Afrika nchini humo AMISOM zimeanzisha mkutano wa siku tatu kutathmini tishio linalotokana na mabomu ya kutengenezwa kienyeji na kuweka mipango ya kukabiliana nalo.
Mkutano huo ulioandaliwa na Tume ya Umoja wa Mataifa ya kuondoa mabomu ya ardhini UNMAS, unalenga kuendeleza uwezo wa kupambana na tishio la mabomu ya kutengenezwa kienyeji nchini Somalia.
Washiriki wa mkutano huo watabadilishana maoni kuhusu mabomu hayo, na kujadili jinsi ya kudhibiti matumizi ya mabomu hayo kwa makundi ya kigaidi kama Al-Shabaab.
Mjumbe maalum wa mwenyekiti wa Umoja wa Afrika anayeshughulikia masuala ya Somalia Bw. Francisco Madeira, amewahimiza washirika wa kimataifa kuendelea kutoa msaada kwa AMISOM na serikali ya Somalia ili kusaidia kupunguza tishio la mabomu hayo kwa watu na vikosi vya usalama nchini Somalia.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |