• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Wakazi wa Beijing wafanya juhudi ya kuhifadhi mfereji mkubwa

    (GMT+08:00) 2017-09-29 17:09:19

    Mfereji wa kaskazini mjini Beijing ni sehemu ya kaskazini ya mfereji mkubwa wa Jinghang unaojulikana duniani. Mfereji mkubwa wa Jinghang ni mfereji uliochimbwa na watu wenye urefu mkubwa zaidi na historia ndefu zaidi duniani, ukiwa na urefu wa kilomita 1794. Mfereji huo umeunganisha mito mitano kutoka upande wa kaskazini hadi kusini, ukiwemo mto Hai, mto Manjano, mto Huai, mto Changjiang na mto Qiantangjiang. Mfereji huo umeshuhudia busara ya wachina kuishi kwa amani na mazingira ya asili katika enzi ya kilimo na kutuachia urithi wa hazina ya utamaduni. Wakazi wa Beijing wamefanya juhudi ya kuhifadhi mfereji huo. Bw. Zhang Hongfeng ni mkazi wa kijiji cha Zhang Xinzhuang cha kitongoji cha Beijing, ambaye alikulia kando ya mfereji mkubwa. Katika miaka ya themanini na tisini ya karne iliyopita, viwanda vingi vilijengwa kando ya mfereji huo na kusababisha uchafuzi wa maji ya mfereji huo. Viumbe katika mfereji huo walikaribia kutoweka, maji ya wakazi wa kando ya mto yalikuwa yanachafuka, huku maji kwenye baadhi ya sehemu za mfereji huo yakikauka. Bw. Zhang amesema,

    "Hatuwezi kuachana na mfereji huo, tulikua kwa kunywa maji ya mfereji huo kuanzia utotoni. Zamani kulikuwa na boti, feri na wavuvi katika mfereji huo. Baada ya hapo, maji yalichafuka, na shughuli zote zilikuwa hazionekeni tena."

    Kufuatia maendeleo ya ujenzi wa mji, serikali ya Beijing imeimarisha usimamizi wa mazingira ya mfereji huo. Sasa mashamba na ardhi oevu za kijiji cha Zhangxinzhuang zilizoko kando ya mfereji wa kaskazini zimejengwa kuwa sehemu ya bustani ya misitu ya mfereji mkubwa. Miti imepandwa kando ya mfereji, maji yamekuwa safi, mfereji wenye mandhari safi ulioko kwenye kumbukumbu ya Bw. Zhang umerejeshwa. Mwanakijiji wa kijiji cha Zhangxinzhuang mwenye umri wa miaka 60 Bw. Wang Youshun pia ameshuhudia mabadiliko ya maji ya mfereji huo. Bw. Wang anasema,

    "Wakati nilipokuwa na umri wa miaka 5 au 6, niliweza kuona samaki nikisimama kando ya mfereji. Nilipokata nyasi za chakula cha nguruwe na kondoo kando ya mfereji huo, nikiwa na kiu nilikuwa naweza kunywa maji ya mfereji huo moja kwa moja. Baada ya kuingia sekondari, kiwanda cha kutengeneza karatasi na cha kemikali vilijengwa kando ya mfereji na kuchafua maji. Baada ya kiwanda cha karatasi kufungwa, maji yalianza kuwa safi kidogo. Baada ya kiwanda cha kemikali kufugwa, maji yalikuwa mazuri zaidi. Sasa watu wanapenda kuishi katika mazingira mazuri zaidi, mazingira ya bustani hiyo ya misitu ni mazuri sana. Zamani sikutarajia kuwa maji ya mfereji huo yatakuwa safi namna hiyo."

    Hivi sasa, Bw. Zhang Hongfeng anawajibika na kazi ya kufanya doria ya kulinda mazingira ya asili ya sehemu ya mfereji yenye umbali wa kilomita 8. Kila wiki anafanya doria mara kadhaa katika sehemu hiyo, ili kuzuia watu wasimwaga maji machafu au kutupa takataka kwenye mfereji huo. Kufutia kuimarika kwa mtazamo wa kuhifadhi mazingira, wanakijiji wengi wanajitolea kuhifadhi mazingira ya mfereji huo. Usimamizi wa mazingira ya mfereji wa kijiji cha Zhangxinzhuang ni moja kati ya miradi zaidi ya kumi inayotekelezwa na serikali ya eneo la Tongzhou la mji wa Beijing katika usimamizi wa mazingira ya maji. Mkuu wa idara ya mambo ya maji ya eneo la Tongzhou Bw. Fang Yajun anasema,

    "Kuanzia mwaka 2015, kwa mujibu wa mpango, tumefanya kazi ya ujenzi wa mazingira ya maji na kutekeleza miradi zaidi ya kumi ya utoaji wa maji, usimamizi wa mazingira ya maji, kukarabati mfereji na kuzuia mafuriko na kuondoa maji taka. Sifa ya maji ya mfereji katika eneo la Tongzhou imeboreka kidhahiri. Hadi kufikia mwezi wa Juni mwaka huu, maji taka yanayonuka katika sehemu 19 yameondolewa kabisa. Kiwango cha maji katika mfereji wa kaskazini na mfereji wa Tonghui kimeinuliwa kwa kiasi kikubwa. Katika hatua ijayo tutaendelea kutekeleza mpango wetu, ili kuinua mazingira ya maji ya eneo la Tongzhou katika kiwango cha juu zaidi. "

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako