• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Maraia wa China na Marekani wakutana na kupanga uhusiano wa nchi zao katika kipindi kipya

    (GMT+08:00) 2017-11-09 16:56:26

    Rais Xi Jinping wa China leo amemwandalia sherehe kubwa za kumkaribisha mwenzake wa Marekani rais Donald Trump ambaye yupo ziarani hapa Beijing, China. Marais hao pia wamefanya mazungumzo, wakikubaliana kuendelea kuonesha nafasi yao ya uongozi wa kimkakati kwa uhusiano kati ya China na Marekani, kuimarisha mawasiliano katika ngazi mbalimbali, kutumia vizuri mazungumzo manne ya ngazi ya juu, kupanua ushirikiano katika sekta ya uchumi na biashara, majeshi, utekelezaji wa sheria na utamaduni, na kuongeza mawasiliano na uratibu katika masuala makubwa ya kimataifa na kikanda, ili kuhimiza uhusiano kati ya China na Marekani kupata maendeleo zaidi.

     Leo asubuhi, China ilimpokea rais Donald Trump wa Marekani kwa sherehe ya ngazi ya "zaidi ya ziara ya kitaifa", na baadaye marais wa China na Marekani wakaanza rasmi mazungumzo yao mbalimbali, makubwa ama madogo, ambayo yamepita muda uliowekwa. Mada walizozungumzia zinahusu uhusiano kati ya China na Marekani, na masuala ya kimataifa na ya kikanda wanayofuatilia kwa pamoja. Kwenye mkutano na waandishi wa habari baada ya mazungumzo yao, rais Xi alisema mazungumzo hayo ni ya kiujenzi na kupata matunda mengi.

    "Ziara ya rais Trump nchini China ni ziara ya kihistoria yenye mafanikio, na mikutano yetu imedhihirisha na kuweka mpango wa jinsi ya kukuza uhusiano kati ya nchi zetu. Tunapenda kushirikiana na Marekani kufuata makubaliano tuliyofikia, kuhimiza uhusiano wa nchi zetu kupata maendeleo zaidi na kunufaisha nchi na watu wake."

    Kwenye mazungumzo, rais Xi amesema sekta ya usalama wa kidiplomasia inahusu maendeleo ya jumla ya uhusiano kati ya China na Marekani na kiwango cha kuaminiana kimkakati kati ya nchi hizo. Na ameongeza kuwa suala la Taiwan ni suala lenye umuhimu mkubwa na unyeti zaidi katika uhusiano kati ya China na Marekani, pia linahusu msingi wa kisiasa katika uhusiano wa nchi zao, na kwamba China inataka Marekani iendelee kufuata kanuni ya kuwepo kwa China moja, kuepusha uhusiano kati ya nchi hizo usisumbuliwe na suala hilo. Pia uhusiano kati ya majeshi ya China na Marekani unatakiwa kuwa sekta ya utulivu katika uhusiano kati ya China na Marekani na kwamba bahari ya Pasifiki ni kubwa vya kutosha kwa China na Marekani kwa pamoja, na maslahi ya pamoja ya nchi hizo mbili katika Asia na Pasifiki ni mengi kuliko tofauti, na pande hizo zinapaswa kufanya ushirikiano mzuri.

    Takwimu zinaonesha kuwa katika miaka 30 iliyopita, thamani ya biashara kati ya China na Marekani imeongezeka kwa mara zaidi ya 200, hivi sasa uhusiano wa kiuchumi na kibiashara umechukua nafasi ya kimsingi na msukumo kwa uhusiano kati ya China na Marekani. Wakati ziara hiyo, nchi hizo mbili zimesaini mikataba yenye thamani ya dola za kimarekani zaidi ya bilioni 250. Akizungumza na waandishi wa habari, rais Xi anasema,

    "Tunaona China na Marekani zikishika nafasi mbili za mwanzo kwa ukubwa wa uchumi duniani na zinazochangia zaidi ukuaji wa uchumi wa dunia, zinapaswa kupanua ushirikiano katika biashara na uwekezaji, kuongeza uratibu kuhusu sera za uchumi wa jumla, na kuhimiza uhusiano wa kiuchumi na kibiashara kuendelezwa vizuri, kwa utulivu na uwiano. Kuna haja ya kupanga mpango wa baadaye wa ushirikiano wa kiuchumi kati ya China na Marekani, kujadili kwa kina kuhusu jinsi ya kushughulikia ukosefu wa uwiano wa kibiashara, kulegeza masharti ya uuzaji bidhaa nje, kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa makampuni na kufungua masoko kwa nje, kupanua ushirikiano katika sekta za nishati, miundombinu na ujenzi wa Ukanda Mmoja, Njia Moja. China pia imetangaza hatua za kufungua masoko yake kwa nje, na kuonesha vya kutosha maeneo makubwa ya ushirikiano wa kiuchumi na kibiashara kati ya China na Marekani yatakavyonufaisha wananchi wao."

    Mbali na ajenda ya uchumi na biashara, suala la nyuklia la Peninsula ya Korea pia limejadiliwa kwenye mazungumzo ya leo. Marais hao wawili wamekubali kuongeza mawasiliano na uratibu katika masuala makubwa ya kikanda na ya kimataifa, na kuhimiza masuala husika kutatuliwa mwafaka.

    "Kuhusu suala la nyuklia la Peninsula ya Korea, sisi tumesisitiza msimamo wa kufanya Peninsula hiyo iwe sehemu isiyo na silaha za nyuklia, kulinda mkataba wa kutoeneza silaha za nyuklia wa kimataifa. Pande hizo zitaendelea kutekeleza kikamilifu maazimio mbalimbali ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, na kufanya juhudi kufanya suala la nyuklia la Peninsula ya Korea litatuliwe kwa njia ya mazungumzo. Pia tunapenda kujadiliana na pande nyingine kwa lengo la kufikia usalama wa kudumu katika Peninsula hiyo na Asia Mashariki."

    Marais hao wawili pia wamekubaliana kuwa uhusiano mzuri wa China na Marekani sio tu unaendana na maslahi makuu ya wananchi wa nchi hizo mbili, pia ni matarajio ya pamoja ya jumuiya ya kimataifa. Rais Donald Trump anasema,

    "Marekani na wenzi wengine kama China tuna fursa nyingi, na tunaweza kuhimiza amani, usalama na ustawi wa dunia nzima. Katika kipindi hicho maalumu cha sasa, tuna fursa maalumu, tunabeba majukumu makubwa. Natarajia tusitumie vibaya fursa hizo, na kufanya nchi zetu na wananchi wetu kupata maendeleo kwa pamoja. Napenda kuona nchi zetu mbili zinajenga uhusiano wenye nguvu zaidi, na kuongeza urafiki na uhusiano kati ya nchi zetu na wananchi wetu."

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako