Bei za bidhaa za mafuta ya petroli na dizeli zimepanda kuanzia leo ikilinganishwa na bei hizi mwezi uliopita. Katika taarifa yake kupitia matangazo kwa vyombo vya habari jana, Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) ilisema bei kikomo za bidhaa mbalimbali za mafuta zinaanza kutumika nchi nzima kuanzia leo.
Taarifa ilisema bei za jumla na rejareja kwa mafuta ya aina zote yaliyoingizwa nchini kupitia bandari ya Dar es Salaam, yaani petroli, dizeli na mafuta ya taa zimeongezeka ikilinganishwa na toleo lililopita la Desemba 2017.
Kwa mwezi Januari 2018, bei za rejareja za petroli imeongezeka kwa Sh 8 kwa lita (sawa na asilimia 0.35), dizeli Sh 34 kwa lita (sawa na asilimia 1.71) na mafuta ya taa zimeongezeka kwa Sh 89 kwa lita (sawa na asilimia 4.57).
Kwa kulinganisha na toleo la mwezi uliopita, bei za jumla za petroli zimeongezeka kwa Sh 7.56 kwa lita (sawa na asilimia 0.37), dizeli Sh 33.97 kwa lita (sawa na asilimia 1.81) na mafuta ya taa Sh 88.73 kwa lita (sawa na asilimia 4.85).
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |