Shirika la kuhudumia wakimbizi la Umoja wa mataifa UNHCR limesema litashirikiana na wadau mbalimbali kuwasaidia wakimbizi walioko nchini Rwanda kukabiliana na tatizo la upungufu wa chakula.
Akiongea na wanahabari baada ya kutembelea kambi ya wakimbizi ya Gihembe, iliyoko katika wilaya ya Gicumbi, Kamishna mkuu wa UNHCR Bw. Filippo Grandi amesema watatumia mbinu mpya, ikiwa ni pamoja na kushirikiana na Shirika la mpango wa chakula duniani WFP kuhusu msaada wa chakula.
Wakimbizi walioongea na wanahabari wamesema lishe kwao ni tatizo kubwa, na familia nyingi za wakimbizi huwa zinapata mlo mmoja tu kila siku. Wizara ya usimamizi wa majanga na mambo ya wakimbizi ya Rwanda imesema kambi ya Gihembe ina wakimbizi elfu 12 kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Ziara ya Bw. Grandi inafuatia mgomo uliofanywa na wakimbizi wakipinga uamuzi wa Shirika la mpango wa chakula duniani WFP kupunguza mgao wa chakula.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |