Tanzania inaendesha zoezi la miezi miwili la kutoa elimu juu ya bidhaa feki kufuatia ongezeko la bidhaa zisizofikia viwango vya ubora zinazoingizwa nchini humo.
Taarifa ya pamoja iliyotolewa na shirika la viwango la Tanzania TBS na tume ya ushindani ya Tanzania FCC inasema kampeni hiyo inalenga kutoa elimu kwa umma juu ya kazi za taasisi hizo mbili za kiserikali katika kudhibiti kukithiri kwa bidhaa zisizokuwa na ubora.
Afisa mawasiliano mwandamizi wa FCC Frank Mdimi alisema maofisa wa kutoka FCC na TBS watafanya kazi kwa pamoja katika kipindi chote cha kampeni hiyo akiongeza kuwa katika kipindi chote hicho wataufikia umma kupitia radio na televisheni na kwa kufanya mikutano na wafanyabiashara.
Naye Afisa mawasiliano mwandamizi wa TBS Roida Andusamile alisema watumiaji wa bidhaa wana uelewa mdogo kuhusu majukumu ya TBS na FCC katika mapambano dhidi ya bidhaa feki na bidhaa zisizokidhi viwango.
Taasisi mbili hizo, zote ziko chini ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ya Tanzania na zina jukumu la kusimamia usawa wa ushindani katika biashara na ubora wa bidhaa.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |