• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • China iko tayari kukabiliana na uwekezano wowote kufuatia Marekani kutishia kuongeza vikwazo zaidi dhidi ya uwekezaji wa China

    (GMT+08:00) 2018-04-26 17:13:44

    Wizara ya Biashara ya China imesema China iko tayari kujiandaa kwa hali mbaya zaidi na kukabiliana na hatua yoyote inayoweza kuchukuliwa na Marekani ya kuweka ukomo dhidi ya uwekezaji wa China.

    Afisa wa Wizara ya Fedha ya Marekani amedokeza kuwa, serikali ya nchi hiyo inatathmini uwezekano wa kuzindua Sheria ya Mamlaka ya Dharura dhidi ya uwekezaji wa China na kuweka vikwazo vipya dhidi ya uwekezaji wa China kwenye sekta ya sayansi na teknolojia. Msemaji wa Wizara ya Biashara ya China Gao Feng amesema China inapinga kithabiti aina zote za sera ya upande mmoja na vitendo vya kujilinda kibiashara.

    "Kwa miaka mingi, uwekezaji wa kampuni za China nchini Marekani umetoa mchango mkubwa katika kuongeza nafasi za ajira na kuhimiza maendeleo ya kiuchumi ya nchi hiyo. Pia tumegundua kuwa kutokana na ukosefu wa uhakika kwenye mazingira ya uwekezaji, baadhi ya kampuni zimepunguza kasi za uwekezaji wao nchini Marekani, na hata kufuta mipango ya kuwekeza nchini humo, na kuacha soko la Marekani. Marekani inatakiwa kufanya matendo yanayoendana na utaratibu wa maendeleo na mkondo wa maendeleo ya uchumi wa dunia, kitu ambacho pia kitainufaisha nchi hiyo na kusaidia utulivu wa muda mrefu wa uchumi wa kimataifa."

    Bw. Gao Feng amesisitiza kuwa China inasikiliza yanayosemwa na Marekani, na pia kuangalia yanayofanywa na nchi hiyo. China imejiandaa kwa hali mbaya zaidi na iko tayari kukabiliana na uwekezano wowote.

    Takwimu zinaonesha kuwa hadi kufikia mwishoni mwa mwaka 2016, uwekezaji wa moja kwa moja wa China nchini Marekani ulifikia dola za kimarekani 109, na umehusisha sekta za huduma, utengenezaji, soko la nyumba, hoteli, teknolojia ya habari na mawasiliano, burudani na huduma za kifedha. Miradi ya uwekezaji ya China iko katika majimbo 46 ya Marekani, na kutoa nafasi za ajira laki 1.41 kwa watu wa nchi hiyo.

    Kinachostahili kufuatiliwa ni kuwa, jana nchi saba wanachama wa Shirika la Biashara Duniani WTO waliungana na China na kueleza ufuatiliaji wao na kusikitishwa na uamuzi wa hivi karibuni uliofanywa na Marekani wa kuongeza ushuru dhidi ya bidhaa za chuma cha pua na alumini zinazoagizwa kutoka nchi hizo nchini Marekani kwa mujibu wa kipengele cha 232. Vilevile tarehe 16 mwezi huu, Umoja wa Ulaya umeiandikia barua Marekani na kutaka kufanya mazungumzo kati ya pande hizo mbili kuhusu kipengele cha 232. Umoja wa Ulaya umesema kwenye barua hiyo kuwa Marekani inakichukulia kipengele cha 232 kuwa ni hatua ya usalama wa kitaifa, lakini hali halisi ni hatua ya kujilinda. Bw. Gao Feng anasema,

    "Hadi sasa, mbali na Umoja wa Ulaya, nchi wanachama wa WTO zikiwemo Russia, India, Uturuki na Thailand pia wameeleza madai yao ya kufanya mazungumzo na Marekani. Tarehe 19, mwezi huu, Umoja wa Ulaya uliiandikia barua tena Marekani na kutaka kuungana na China kutoa malalamiko kwa WTO."

    Bw. Gao amesisitiza kuwa Marekani inatumia kisingizio cha usalama wa taifa kuweka vikwazo dhidi ya uagizaji wa bidhaa za chuma cha pua na alumini kutoka nje, kitendo hicho kimekiuka kanuni na nidhamu husika za WTO, kuharibu mfumo wa pande nyingi, kutishia maslahi halali ya nchi wanachama wa WTO, na kupingwa kwa pamoja na nchi hizo. Ameongeza kuwa China itaungana na nchi nyingine wanachama wa WTO kulinda maslahi yao halali.

    Aidha, Bw. Gao Feng amesema China inatunga mwongozo wa kuongeza uagizaji bidhaa kutoka nje na kuhimiza uwiano wa biashara ya China na nje.

    "Hivi sasa, wizara ya biashara ya China inashirikiana na idara nyingine kutafiti sera na hatua za kuongeza uagizaji bidhaa kutoka nje. Tutapunguza zaidi ushuru wa bidhaa zitakazoagizwa kutoka nje ikiwemo magari na baadhi ya bidhaa za matumizi ya kila siku, kuongeza uagizaji wa bidhaa wanazohitaji zaidi watu wa China na kutoa hatua za kurahisisha biashara. Pia tutajitahidi kuandaa vizuri maonyesho ya kimataifa ya uagizaji bidhaa kutoka nje ya China."

    Bw. Gao Feng amesema kupanua zaidi uagizaji bidhaa kutoka nje kunasaidia kuhimiza uwiano wa matumizi na mapato ya China, na ni hatua muhimu ya hiari ya China ya kufungua soko lake, kujiunga na uchumi wa dunia na kuhimiza mafungamao ya kiuchumi duniani.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako