Ikulu ya Marekani imetangaza kuwa waziri wa mambo ya nje wa Marekani Bw. Mike Pompeo atakutana na naibu mwenyekiti wa kamati kuu ya chama cha leba cha Korea Kaskazini Bw. Kim Yong Chol aliyeko ziarani nchini Marekani wiki hii. Msemaji wa ikulu ya Marekani Bibi Sarah Sanders amedokeza kwenye taarifa kuwa ujumbe wa Marekani unaoongozwa na mwanadiplomasia mkongwe Sung Kim, umekutana na maofisa wa Korea Kaskazini kwenye eneo salama la mpakani kati ya Korea Kusini na Korea Kaskazini, na mikutano mingine itafanyika wiki hii. Imefahamika kuwa mkutano kati ya rais Donald Trump wa Marekani na kiongozi wa Korea Kaskazini Bw. Kim Jong Un huenda utafanyika Juni 12 nchini Singapore kama ilivyopangwa, baada ya rais Trump kutangaza kuufuta mkutano huo Alhamisi iliyopita na kuishutumu Korea Kaskazini kuonesha "hasira kubwa na uhasama wa wazi".
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |