Waziri mkuu wa Uingereza Bibi Theresa May amemwambia mwenzake wa Israel Bw. Benjamin Netanyahu kuwa Uingereza inaunga mkono kithabiti makubaliano ya nyuklia ya Iran, licha ya Marekani kujitoa kwenye makubaliano hayo.
Akizungumza na Bw. Netanyahu Bibi May amesema kutekeleza makubaliano ya nyuklia ya Iran ni njia bora ya kuizuia nchi hiyo kutengeneza silaha za nyuklia. Mawaziri wakuu wa nchi hizo mbili pia wamekubaliana kuhusu hitaji la kuzuia shughuli za Iran za kuvuruga utulivu wa Mashariki ya Kati.
Mkutano huo umefanyika baada ya Bw. Netanyahu kufanya majadiliano kuhusu suala hili na rais Emmanuel Macron wa Ufaransa na Chansela wa Ujerumani Angela Merkel, ambao wote wameeleza kuunga mkono makubaliano hayo.
Hata hivyo msemaji wa Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki IAEA amesema Iran imelifahamisha kuhusu mipango yake ya kuongeza uwezo wa kurutubisha madini ya uranium. Mapema ya wiki hii kiongozi mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei alitaka kufanyika kwa maandalizi ya kuongeza uwezo wa kurutubisha madini ya uranium, kama makubaliano ya nyuklia ya Iran yakivunjwa.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |