Wakulima 17 wa mashamba ya miwa wilayani Kilosa nchini Tanzania wamenufaika na urasimishaji mashamba kwa kutumia hatimiliki za kimila kukopa Sh milioni 550 kutoka Benki ya Maendeleo ya Wakulima; imeelezwa.
Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, Adam Mgoyi amesema hayo mjini hayo alipokuwa akizungumzia manufaa ya urasimishaji ardhi na mashamba wilayani humo unaoratibiwa na Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (Mkurabita).
Alisema kupitia Mkurabita na wadau wengine, wilaya ya Kilosa inanufaika na urasimishaji mashamba na ardhi kwa kuwa umekuwa chachu ya maendeleo na kilimo chenye tija kinachoongeza pato la wananchi na halmashauri kwa jumla.
Kwa kipindi cha miaka miwili wakulima 17 wa miwa huko Luhembe wametumia urasimishaji wa ekari zao 6,000 za miwa kupata fursa ya kukopa na hivyo wameongeza uzalishaji wa mavuno.
Bw Mgoyi ametoa mwito kwa taasisi za fedha zikiwamo benki wilayani humo kuendelea kuzitambua hati za hatimiliki za kimila na kuzitumia kama dhamana ya mikopo kwa kuwa ni hati halali za kisheria zinazotolewa na serikali.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |