Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya amesisitiza kuwa vikosi vya Kenya vitaendelea na mapambano dhidi ya kundi la Al-Shabab nchini Somalia hadi amani na utulivu vitakaporejeshwa.
Rais Kenyatta amesema jeshi la ulinzi la Kenya KDF likiwa ni sehemu ya tume ya Umoja wa Afrika nchini Somalia AMISOM, litaendelea na majukumu yao nchini Somalia hadi nchi hiyo itakaporejesha amani, utulivu na utaratibu wa kawaida.
Akiongea kwenye hafla ya uteuzi wa kikundi cha sita cha maofisa wa jeshi waliopewa mafunzo ya miaka mitatu, rais Kenyatta amewaagiza maofisa hao wapya kuenzi mila na desturi ya jeshi la Kenya na kuwa wanajeshi hodari zaidi duniani.
Habari nyingine kutoka Somalia zinasema, vikosi vya usalama vya Somalia jana vilimkamata mpiganaji mmoja wa kundi la Al-Shabab, aliyetuhumiwa kupanga mlipuko wa hoteli ya Sahafi uliotokea Novemba tisa na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 50.
Shirika la Intelijinsia na Usalama la Somalia NISA limesema mpiganaji huyo atapandishwa kizimbani baada ya uchunguzi dhidi yake kumalizika.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |