Wanaharakati wa Sudan Kusini wamesema watafufua mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia ambao umekuwa ukiongezeka nchini Sudan Kusini kutokana na vita ya wenyewe kwa wenyewe na imani za jadi.
Wanaharakati hao kutoka makundi ya wasomi na jumuiya za kiraia wamesema watahamasisha watu wa mashinani kwa lengo la kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.
Nyanthon James Oath, ambaye ni mtafiti wa mambo ya kijinsia katika jumuiya ya washauri bingwa, Sudd Institute, yenye makao yake mjini Juba amesema kampeni ya mwaka mmoja tayari imeanza ili kufahamisha ukatili wanaotendewa wanawake.
Amesema moja ya malengo ya kampeni hiyo ni kupambana na mila zilizopitwa na wakati kuhusu nafasi ya mwanamke katika jamii, kwani ukweli ni kwamba wanawake walio wengi wamekuwa na mchango mkubwa kwenye kufanikisha amani endelevu nchini Sudan Kusini.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |