Timu ya taifa ya raga ya wachezaji 15 kila upande almaarufu Kenya Simbas inalidai Shirikisho la Raga la Kenya (KRU) mamilioni ya fedha ambayo ni mshahara wa mwezi Novemba mwaka 2018. Ripoti zinasema kwamba wachezaji 30 waliozuru jiji la Bucharest mnamo Novemba 3 na kujipima nguvu dhidi ya Romania pamoja na kushiriki mchujo wa mwisho wa kufuzu kushiriki Kombe la Dunia kati ya Novemba 11 na Novemba 23 nchini Ufaransa, wanaidai KRU Sh40,000 kila mmoja. Simbas, ambayo ilimaliza Kombe la Afrika katika nafasi ya pili nyuma ya Namibia mwezi Agosti, ilichabangwa 36-5 na Romania kabla ya kulemewa na Canada (65-19), Hong Kong (42-17) na Ujerumani (43-6).
Canada ilipepeta kila timu katika mchujo huo na kunyakua tiketi ya kushiriki Kombe la Dunia nchini Japan.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |