Ofisa mwandamizi wa Umoja wa mataifa ameipongeza Kenya kwa kutengeneza jahazi kwa kutumia taka za plastiki.
Kaimu mkurugenzi mtendaji wa Shirika la mazingira la Umoja wa mataifa UNEP Bibi Joyce Msuya amesema uvumbuzi huo umeonesha kuwa nchi za Afrika zinaweza kuongoza katika uhifadhi wa mazingira.
Akiongea na wanahabari kwenye uzinduzi wa jahazi la kwanza lililotengenezwa kwa taka za plastiki mjini Nairobi, Bibi Msuya amesema hii ni alama kuwa juhudi zinazohimizwa na jamii zinaweza kutoa suluhu kwa matatizo ya muda mrefu yanayoikabili dunia, na pia imeonesha maendeleo yaliyopatikana nchini Kenya tangu nchi hiyo ipige marufuku mifuko ya plastiki mwaka 2017.
Bibi Msuya amezihimiza serikali za nchi za Afrika ambazo bado hazijachukua hatua madhubuti kuharakisha juhudi zao, na kuongeza kuwa nchi za Afrika kusini mwa Sahara zinatoa tani milioni 170 za taka za plastiki, ambazo zinachangia asilimia 12 ya jumla ya taka hizo kote duniani.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |