Serikali ya Zimbabwe imesema inahitaji msaada wa si chini ya dola za kimarekani milioni 612 ili kuwasaidia wahanga wa kimbunga cha Idai.
Kimbunga hicho kilizikumba sehemu za mashariki na kusini za nchi hiyo na kusababisha vifo na uharibifu mkubwa, na baadaye kufuatiwa na mafuriko yaliyotajwa kuwa ni janga la taifa.
Waziri wa serikali za mitaa, ujenzi na makazi wa Zimbabwe Bw. July Moyo amesema wanahitaji msaada huo kutoka kwa wahisani wa ndani, wa kikanda na wa kimataifa.
Maeneo yaliyotajwa kuhitaji fedha za msaada ni pamoja na chakula na lishe, mawasiliano, makazi ya dharura, usafiri wa maji, afya, elimu na mengine.
Msaada huo unahitajika kwa kipindi kuanzia mwezi huu hadi mwezi Mei mwaka kesho wakati wa msimu mwingine wa mavuno.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |