Wajumbe wa kamati ya bunge ya viwanda, biashara na mazingira nchini Tanzania wameitaka serikali kuchukua hatua za dharura zinazolenga kukabiliana na uharibifu wa misitu nchini humo.
Naibu mwenyekiti wa kamati hiyo Bw. Ali Khamis Masoud amesema hayo wakati akiwasilisha ripoti ya makadirio ya bajeti ya kamati hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2019/2020 kwenye Ofisi ya Makamu wa Rais inayoshughulika na mazingira. Amesema Ziwa Manyara, Jipe na Chala yako kwenye hatari ya kutoweka kutokana na uharibifu wa misitu, na kuongeza kuwa ushahidi uliopo unaonyesha kuwa vitendo vya kibinadamu ndani na kuzunguka vyanzo vya maji ya maziwa hayo ikiwemo ukataji mkubwa wa miti ni moja ya tatizo kubwa.
Amesema katika miaka ya karibuni, Tanzania imeibuka katika orodha ya nchi zinazokabiliwa na uhaba wa maji, na kusisitiza kuwa hatua zichukuliwe kukabiliana na uharibifu wa misitu unaosababishwa na sababu zinazoweza kuzuilika.
Kamati hiyo imeshauri kuwa serikali itenge fedha za kutosha kutoka vyanzo vya mapato vya ndani kwa ajili ya ulinzi wa mazingira.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |