Kocha Felix Oloo anapania kuwategemea pakubwa wanaraga Sheila Chajira, Vivian Akumu na Naomi Amuguni ili kuweka hai matumaini ya timu ya taifa ya Lionesses katika raga ya wachezaja 15 kila upande nchini Afrika Kusini. Kikosi hicho kiliondoka Kenya kuelekea Afrika Kusini kwa mechi za kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia 2021. Michuano hiyo ya mchujo inafanyika Agosti 9 hadi 17 katika uwanja wa Bosman, Johannesburg. Kenya wamepangwa kupepetana na wenyeji Afrika Kusini, Uganda na Madagascar katika jitihada za kuwania tiketi ya kushiriki fainali za Kombe la Dunia zitakazoandaliwa nchini New Zealand. Lionesses watafungua kampeni zao dhidi ya Madagascar kesho Agosti 9 kisha kuchuana na Uganda Lady Cranes kwa mara ya tatu mwaka huu mnamo Agosti 13. Watafunga mechi zao dhidi ya Afrika Kusini Agosti 17. Mshindi wa kivumbi hicho atajikatia tiketi ya Kombe la Dunia moja kwa moja huku mshindi wa pili akilazimika kushiriki mchujo mwingine dhidi ya mojawapo ya timu za Amerika Kusini ili kufuzu.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |