Shirikisho la soka nchini Misri (EFA) limeiandikia barua FIFA kuomba ufafanuzi kuhusiana na kura yao ya tuzo ya The Best FIFA kutoonekana kitu ambacho kimempelekea staa wao Mohamed Salah anayeichezea Liverpool ya England kuona kama nchi yake inataka kumfanya aondoe mapenzi na taifa lake. Kwa kawaida kura za kumchagua mchezaji bora wa FIFA wa mwaka huwa zinapigwa na makocha wa timu za taifa na manahodha na kuwasilishwa FIFA kupitia shirikisho la soka la nchi husika lakini kwa upande wa kura za Misri hazijaonekana zimeenda wapi wakati kulikuwa na MO Salah katika tuzo hizo, kitu ambacho kimeleta wasiwasi. Inadaiwa kuwa MO Salah hajakichukulia poa kitendo hicho na badala yake ameandika ujumbe unaotafsiriwa kama dongo kwa shirikisho lake baada ya kushindwa kumpigia kura Hata hivyo (EFA) limejitetea kwa kudai kuwa nahodha wao Ahmed Elmohamady na kocha wao Shawky Gharib walimpigia kura mchezaji huyo lakini hawajui kwa nini kura zao hazijaonekana katika upigaji kura.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |