Timu ya taifa ya mpira wa voliboli kwa akina dada, Malkia Strikers, wamejikatia tiketi ya kuingia kwenye mashindano ya Olimpiki mwaka huu yatakayofanyika mjini Tokyo, Japan. Malkia Strikers walipata nafasi hiyo baada ya kuitafuna timu ya Nigeria walipokutana katika mashindano ya mataifa ya Afrika kufuzu Olimpiki katika mechi iliyochezwa Yaoundé, Cameroon. Akina dada hao wa Kenya waliingiza mguu mmoja kwenye mashindano hayo ya Japan Jumanne, Januari 7 baada ya kuwanyuka Cameroon seti tatu kwa mbili. Kufikia Alhamisi, Januari 9, timu hiyo ya Kenya ilikuwa imebaki na Nigeria na walipoingia uwanjani wakaitafuna kama mnofu wa nyama. Malkia walianza kwa kishindo baada ya kuinyuka Nigeria 25-15 kwenye seti ya kwanza, raundi ya pili wakawapepeta 25-21 na kisha kuwamalizia na 25-21. Sasa timu hiyo itashiriki Olimpiki tena baada ya miaka 16 kwani mara ya mwisho kushiriki ilikuwa mwaka 2004 nchini Ugiriki.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |