Rais wa Porto Jorge Nuno Pinto da Costa amesema kwamba mlinda mlango Iker Casillas anatarajia kustaafu soka, siku moja baada ya nahodha huyo aliyeisadia Hispania kubeba kombe la dunia Afrika Kusini mwaka 2010 kutangaza kuwania urais wa Shirikisho la Soka la Hispania (RFEF). Casillas, mwenye miaka 38, alitarajiwa kutundika daluga baada ya kutangaza nia lakini hajathibitisha kama kweli atafanya hivyo. Casillas, aliyejiunga na Porto mwaka 2015 na kuugua ugonjwa wa moyo mwezi wa Aprili ambapo hakuweza kucheza tena mechi, anachukuliwa kama mmoja wa walinda mlango nguli katika kizazi chake. Amecheza mara 167 katika timu ya Hispania, pia ameshinda makombe mawili ya mabingwa wa Ulaya mwaka 2008 na 2012, na kucheza zaidi ya mara 700 katika Real Madrid, ambako ameshinda mataji matano ya La Liga na Ligi ya Mabingwa mara tatu.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |