Bingwa wa dunia wa Global Boxing Council, Ibrahim Class amefichua kuwa masuala ya fedha ndio yaliyomkimbiza kwa sasa. Class, aliyeacha gumzo kwenye pambano lake la Novemba 25, 2017 lililopigwa Uwanja wa Uhuru Dar es Salaam kwa kumchakaza Msauzi, Koos Sibiya na kutwaa ubingwa wa dunia uzani wa Super Feather amesema aliamua kujiweka kando kwa muda mrefu kutokana na maslahi kiduchu. Bondia huyo ambaye tangu Juni 16, 2019 alipozichapa na Israel Kammwamba hajaonekana tena ulingoni, amebainisha kwamba maslahi kiduchu ndiyo chanzo kwani alikuwa anapewa mapambano ya fedha ndogo, hela hakuna ndio sababu hajapigana muda mrefu. Hata hivyo bondia huyo ambaye ananolewa na kocha, Habib Kinyogoli (Master) amebainisha kwamba hivi sasa anajipanga upya na atakaporejea ulingoni itakuwa ni mwendo wa mataji ya ubingwa.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |