Chansela wa Ujerumani, Angela Merkel, amethibitisha kwamba upo uwezekano mkubwa kwa Ligi Kuu ya taifa hilo (Bundesliga) kuanza tena mwezi huu. Kutimia kwa hilo kutafanya Bundesliga kuwa ya kwanza miongoni mwa Ligi Kuu za bara Ulaya kuanza upya baada ya shughuli za michezo muhula huu kuvurugwa na corona. Waendeshaji wa kivumbi hicho (DFL) wametoa mpangilio utakaofuatwa na tarehe kamili ya kurejelewa kwa kampeni za gozi hilo. Mechi zote zilizosalia katika kalenda ya Bundesliga msimu huu zitasakatiwa ndani ya viwanja vitupu bila mashabiki. Zikisalia mechi tisa pekee kwa muhula huu kutamatika rasmi, Bayern Munich ambao ni mabingwa watetezi wa Bundesliga wanaselelea kileleni mwa jedwali kwa alama nne zaidi kuliko Borussia Dortmund. Mwenyekiti wa Bayern, Karl Heinz Rummenigge amesema, angependa kuwashukuru wanasiasa kwa maamuzi yao ya kihistoria ambao yanatoa fursa kwa kivumbi cha Bundesliga kukamilishwa msimu huu.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |