Wakati nafasi pekee ya timu ya taifa ya ngumi za ridhaa Tanzania kushiriki Olimpiki ikisalia kwenye mashindano ya dunia, timu hiyo imepiga hodi kwa mkuu wa majeshi, Jenerali Venance Mabeyo kuomba sapoti. Mabondia wa timu hiyo watashiriki mashindano ya dunia mjini Paris, Ufaransa kusaka viwango vya kufuzu Olimpiki ya 2021 nchini Japan. Timu hiyo awali ilikuwa ishiriki mashindano ya dunia mwezi huu lakini kutokana na janga la virusi vya corona, mashindano hayo yamesogezwa mbele hadi mwakani. Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ngumi za Wazi (OBFT), Lukelo Wililo amesema kuwa baada ya mabadiliko hayo, wameandaa programu mpya ya mabondia ambayo ni ya muda mrefu. Amesema katika programu hiyo, wanatarajia kuwa kambini kwa kipindi cha miezi minane hadi 10 mfululizo, hivyo wako mbioni kuomba sapoti ya mkuu wa Majeshi, Jenerali Mabeyo ili awasaidie kambi. Lukelo ameeleza kuwa wanaamini watakapowaweka kwenye kambi ya muda mrefu mabondia wa timu hiyo, watafanya vizuri kwenye mashindano ya dunia.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |