Wakati Kocha Hamis Mwakinyo anayemnoa bondia Hassan Mwakinyo akitarajia mafanikio mapya kwa mwanamasumbwi huyo, promota aliyemtambulisha Mwakinyo duniani, Rashid Nassoro (Chid) amemtajia mambo matatu ambayo anaamini yatamrejesha kwenye rekodi za ubora kimataifa. Chid ambaye aliambatana na Mwakinyo kwenye pambano la Uingereza dhidi ya Sam Eggington ambalo lilimtangaza na kumpandisha hadi nafasi ya 16 kutoka ya 178 duniani mwaka juzi, amesema hatakiwi kucheza na mabondia wa Tanzania kwa sasa kama anahitaji kurudi kwenye ubora, kwani hata akishinda hawezi kupanda kwenye ubora. Mwakinyo sasa ni bondia wa 78 duniani katika uzani wa super welter baada ya kuporomoka hivi karibuni katika 'renki' ya dunia, ingawa kwa Tanzania amesalia kuwa namba moja kwenye uzani huo na nne katika orodha ya mabondia kwenye kila uzani. Amemshauri kupigana na bondia wa kiwango kama hicho kutoka nje ya nchi. Hata hivyo, kocha wake ameeleza kuwa bado wanaamini Mwakinyo atarudi katika kiwango bora akisisitiza kuwa amekuwa katika mazoezi na anachosubiri ni pazia la michezo lifunguliwe.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |