Kwa mujibu wa taarifa ya FAO iliyotolewa wiki jana mjini Roma Italia, kati ya nchi 29 zilizokumbwa na nzige hao waharibufu, 26 zimefanikiwa kuwadhibiti lakini tatu bado zinapambana zikiwemo Kenya , Somalia na Ethiopia.
Hata hivyo shirika hilo linatumai kwamba katika siku chache zijazo zitasalia nchi mbili na ndani ya wiki tatu Kenya na Ethiopia nazo zitajikomboa kwa kiasi kikubwa.
Pamoja na mafanikio hayo Cyril Ferrand kiongozi wa FAO wa masuala ya mnepo katika eneo la Afrika Mashariki ameonya kwamba nchi hizo zinapaswa kujitahidi kwani tishio la kuzuka upya mzunguko mwingine wa nzige wa jangwani mwishoni mwa mwaka huu bado lipo.
Ameongeza kuwa miongoni mwa nchi zote 29 zilizokumbwa na nzige wa jangwani mwaka huu Kenya ndio iliyoathirika vibaya zaidi baada ya kutoshuhudia nzige kwa miaka 70 ikifuatiwa na Ethiopia, Somalia na Sudan Kusini. Juhudi kubwa za FAO kwa kushirikiana na wizara husika za kilimo na chakula katika nchi zilizoathirika zimefanikisha kuokoa karibu ekari laki sita Afrika Mashariki na kuua nzige bilioni 400 hatua iliyozuia uharibifu mkubwa wa mazao.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |