• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Internet yawa moja ya maeneo ambayo ni fursa ya maendeleo kwa watumiaji

    (GMT+08:00) 2016-11-16 10:48:33

    Mkutano kuhusu maendeleo ya internet duniani umefunguliwa leo katika mji wa Wuzhen, Mkoani Zhejiang kusini mwa China. Mkutano huu wa kila mwaka unafanyika wakati China inapata maendeleo ya kasi kwenye teknolojia ya mawasiliano na habari, na inashirikiana na nchi mbalimbali za Afrika kupiga hatua kwenye eneo hilo. Kauli mbiu ya mkutano wa mwaka huu ni "Uvumbuzi unaoeleta maendeleo ya kunufaisha wote – kujenga jamii yenye mustakbali wa pamoja kwenye mtandao wa internet ".

    China ambayo inapata maendeleo ya kasi kwenye teknolojia ya habari na mawasiliano imekuwa mstari wa mbele kuchangia maendeleo yake na ya nchi rafiki za Afrika. Makampuni hodari ya teknolojia ya habari na mawasiliano ya China, kama Huawei na ZTE, yanashirikiana na nchi za Afrika kuendelea teknolojia ya habari na mawasiliano, ikiwa ni pamoja na kujenga miundo mbinu ya mawasiliano na kubadilishana ujunzi na teknolojia na nchi za Afrika.

    Uzoefu wa China katika eneo hilo unatokana na maendeleo yanaonekana kwenye idadi ya watumiaji wa mtandao wa internet, ambayo mwaka jana ilikuwa watu milioni 688, ikimaanisha karibu mmoja kati ya wachina wawili wanaunganika na mtandao huo. Hata njia za utumiaji wa internet zimebadilika kutoka kutumia kompyuta za mezani, hadi kutumia kupitia njia za mawasiliano ya kuhama kama vile simu na Ipad.

    Mwanzoni internet ilitumika zaidi kwa mawasiliano, lakini sasa mbali na mawasiliano, internet imefikia hatua ya kuwa njia ya kufanya biashara, kutoa elimu, burudani, huduma za fedha na hata kusaidia kusimamia mambo ya utawala kwenye baadhi ya maeneo. Sasa internet imekuwa ni moja ya sekta muhimu za uchumi kwa China, na kwa mwaka 2014 thamani yake ilichukua asilimia 7 ya thamani ya jumla ya uzalishaji nchini China.

    Kumekuwa na dalili nzuri za maendeleo ya mtandao wa internet katika nchi za Afrika, licha ya kuwa bado internet haijawa sekta kubwa kiuchumi. Tanzania kwa mfano, hivi karibuni mamlaka ya Usimamizi wa Mawasiliano ya Tanzania (TCRA), ilitoa takwimu zinazoonyesha kuwa ni watanzania milioni 39 kati ya watanzania wote milioni 47 wanatumia simu za mkononi. Wote hao wanaweza kutumia huduma ya internet kama wakiwa na simu zinazofaa. Kati ya wateja milioni 39, ni wateja milioni 17 wanaotumia mtandao wa internet kupitia simu aina ya smartphone.

    Licha ya takwimu hizo za kutia moyo, matumizi ya mtandao wa internet nchini Tanzania bado yapo kwenye kiwango cha msingi. Kwa sasa matumizi makubwa zaidi ni mawasiliano na kutafuta habari. Bado internet haijaanza kutumiwa vya kutosha kama njia ya kujiletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Hata hivyo idadi ya watumiaji wanaofikiwa na internet na maeneo waliko, vinafanya mtandao wa internet uwe ni eneo lenye fursa ya maendeleo.

    Hata hivyo fursa hii imekuja na changamoto zake, ambazo zinaonyesha udhaifu kwenye usimamizi wa utumiaji wa mtandao wa internet. Katika miaka ya hivi karibuni nchi mbalimbali za Afrika zikitunga mfululizo wa sheria za kudhibiti utumiaji wa mtandao wa internet. Hatua hii inatokana serikali za nchi za nchi mbalimbali kuwa na hofu kutokana na matumizi mabaya ya teknolojia hiyo, kama vile kuwa jukwaa la kashfa, upotoshaji na kutishia utulivu na masikilizano ya jamii.

    Tanzania kwa mfano imepitisha sheria mbili zinazotajwa kulenga kulinda usalama kwenye mtandao wa internet. Moja ni sheria kuhusu makosa ya mtandao wa Internet ya mwaka 2015, na ile ya huduma ya vyombo vya habari ya mwaka 2016 iliyopitishwa mwezi huu. Sheria hizo zinaonyesha kuwa bado kuna changamoto kwenye usimamizi wa utumiaji wa mtandao wa internet.

    Maendeleo kwenye maeneo ya kuendeleza miundo mbinu na matumizi ya internet, pamoja na usimamizi wa kisheria wa utumiaji wa mtandao wa internet vitafanya internet iwe na manufaa makubwa zaidi kwa watu wa nchi mbalimbali za Afrika.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako