CORONA: Mohamed Salah apimwa na kuonekana sasa hana maambukizi ya Corona
2020-11-23 16:47:24| cri

Mshambuliaji wa klabu ya Liverpool na timu ya taifa ya Misri, Mohamed Salah amepimwa na vipimo vimeonesha hana maambukizi ya ugonjwa wa Corona alioupata juma lililopita wakati akijandaa na michezo ya kufuzu AFCON mwaka 2021. Kocha wa klabu ya Liverpool, Jurgen Klopp amethibitisha kuwa Salah hana maambukizi ya COVID-19. Salah atafanyiwa vipimo viwili vingine kutoka Shirikisho la soka barani Ulaya,. Vipimo hivyo ni sehemu ya maandalizi ya mchezo ujao wa liverpool dhidi ya Atalanta kutoka nchini Italia kwenye michuano ya UEFA. Ikumbukwe kuwa siku ya jumatatu tarehe 16 mwezi huu, MO Salah alifanyiwa vipimo na kukutwa na ugonjwa wa korona baada ya kuhudhuria sherehe ya kaka yake siku ya Ijumaa tarehe 13 mwezi huu nchini Misri na hata alipofanyiwa vipimo tena jumatano tarehe 18 mwezi huu alikutwa na ugonjwa huo. Salah tayari amekosa michezo miwili ya kufuzu AFCON 2021 dhidi ya Togo kwa ngazi ya timu ya taifa na kuukosa mchezo ambao klabu yake ya Liverpool ilipata ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Leicester City. Kocha wa Liverpool, Jurgen Klopp pia amethibitisha winga Xhedran Shaqiri amepata maumivu kwenye kifundo chake cha mguu akiwa anaichezea timu yake ya taifa ya Switzerland hivyo anataraji kuwa nje kwa takribani zaidi ya wiki moja.