SOKA: Simba yaelekea Nigeria kwa ajili ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Plateau United
2020-11-25 16:11:52| cri

Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba jana Novemba 24 wametia timu nchini Ethiopia ikiwa ni safari ya kuelekea Nigeria kwa ajili ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Plateau United. Simba imeondoka Bongo kupitia Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro ikiwa ni safari ya kuwafuata wapinzani hao.Msafara huo wenye wachezaji 24 pamoja na benchi la ufundi leo Jumatano wanatarajia kuanza safari ya kuelekea Abuja, Nigeria. Kikosi hicho kinachoongozwa na Kocha Mkuu, Sven Vandenbroeck kinatarajiwa kukutana na Plateau United kati ya Novemba 27-29 ikiwa ni mchezo wa awali na mchezo wa marudio unatarajiwa kuchezwa Dar es Salaam, Uwanja wa Mkapa. Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara amesema kuwa hesabu zao ni kuweza kutinga hatua ya nusu fainali kwenye ligi hiyo yenye ushindani mkubwa.