China yahimiza huduma bora za kuwaangalia watoto baada ya muda wa masomo shuleni
2021-05-06 20:45:14| Cri

Nchini China shule za msingi na sekondari huwa zinamaliza masomo saa tisa na nusu alasiri, wakati ambao wazazi wengi hawajamaliza kazi na hivyo hawana nafasi ya kwenda kuwachukua watoto wao shuleni.

Ili kutatua changamoto hiyo, mikoa mingi ya China imetoa sera ya huduma ya kuwaangalia watoto baada ya muda wa masomo shuleni, ambayo inazitaka shule zibebe majukumu ya uangalizi wa watoto baada ya masomo, ili wazazi waweze kuendelea na kazi yao bila wasiwasi.

Kuboresha huduma za shule baada ya masomo, si kama tu ni sehemu ya lengo la kujenga mfumo wa elimu yenye ubora wa juu lililowekwa kwenye Mpango wa 14 wa Maendeleo ya Miaka mitano na Ruwaza ya Maendeleo ya Mwaka 2035, bali pia ni hatua muhimu ya kufikia matarajio ya wananchi.

Mapema mwaka 2017, idara ya elimu ilitoa mwongozo wa kuboresha huduma kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari baada ya muda wa masomo, ikizitaka shule za msingi na sekondari zijitume kubeba majukumu ya kuhudumia wanafunzi baada ya masomo. Mwezi Februari mwaka huu, Wizara ya Elimu ya China ilitoa agizo la kuhakikisha huduma za shule za elimu ya lazima kwa wanafunzi baada ya masomo zinapatikana kila mahali nchini kote, na kuitaka kila shule itekeleze kwa makini.