Mashairi Yaliyopamba Moto katika Enzi ya Tang
中国国际广播电台

      
Enzi ya Tang ni kipindi muhimu katika historia ya China. Katika kipindi hicho uchumi ulistawi, jamii ilikuwa tulivu, utamaduni na sanaa viliendelea kwa haraka na hasa mashairi yalikuwa yamepamba moto. Kutunga mashairi kulikuwa ni maisha muhimu ya wasomi katika Enzi ya Tang. Kitabu kiitwacho “Mkusanyiko wa Mashairi ya Enzi ya Tang” kimekusanya mashairi karibu elfu 50 yaliyoandikwa na washairi zaidi ya elfu mbili na mia tatu.

Maendeleo ya mashairi ya Enzi ya Tang yanaweza kugawanyika katika vipindi vinne vya enzi hiyo, navyo ni kipindi cha mwanzo, kipindi cha ustawi, kipindi cha katikati na kipindi cha mwisho.

Kipindi cha mwanzo (618—712). Katika kipindi hiki waliibuka “washairi hodari wanne”, nao ni Wang Bo, Yang Jong, Lu Jielin na Luo Binwang ambao waliweka kanuni za mashairi ya kale yenye mistari maalumu na kila mstari uwe na maneno maalumu yaani maneno matano au maneno saba. Kutokana na juhudi zao mashairi hayakuwa ya burudani tena ndani ya kasri la kifalme, bali yamekuwa yakieleza maisha halisi ya wananchi.

Kati ya mwaka 712 hadi mwaka 762 kilikuwa ni kipindi cha ustawi cha Enzi ya Tang. Katika kipindi hiki uandishi wa mashairi ulipamba moto. Kulikuwa na mada nyingi za mashairi zikielezea uzuri wa maumbile, kusifu mashujaa na kueleza hisia za masikitiko. Washairi walikuwa wakiandika mashairi katika mazingira ya uhuru na kukifanya kipindi hiki kifikie kilele cha mashairi katika historia ya China.

Katika kipindi hiki cha ustawi cha Enzi ya Tang, washairi wakubwa walikuwa ni Li Bai, Du Fu, Wang Wei, Meng Haoran, Gao Shi na Cen Can. Kati ya hao Li Bai na Du Fu ndio wawakilishi wa washairi wa kipindi hiki, mashairi yao yameathiri sana mashairi ya hapo baadaye.

Katika kipindi cha Katikati cha Enzi ya Tang (762—872) washairi walio maarufu zaidi ni Bai Juyi, Yuan Zhen na Li He. Bai Juyi alikuwa hodari wa kuandika mashairi ya kudhihaki utawala wa kutoza kodi kubwa, kupinga vita na kuwaponda matajiri wenye madaraka, na alijitahidi kutumia lugha rahisi. Mashairi yaliwapendeza sana wasomaji.

Li He alikuwa na maisha mafupi, aliishi zaidi ya miaka 20 tu. kutokana na kuwa maisha yake yalikuwa magumu na tumaini lake liligongwa mwamba, mashairi yake yalijaa huzuni.

Kipindi cha mwisho cha Enzi ya Tang (827—859) ni kipindi ambapo cha washairi Li Shangyin na Du Mu walikuwa katika kilele cha kuandika mashairi. Mashairi ya Du Mu, mengi yalikuwa yakionesha nia yake ya kisiasa, na mashairi ya Li Shangyin mengi yalikuwa yakionesha masikitiko na simanzi kutokana na usumbufu wake alipokuwa na wadhifa.