Mwandishi Mkubwa wa Tamthilia Guan Hanqing
中国国际广播电台

     Katika Enzi ya Yuan, Guan Hanqing alikuwa mwandishi mkubwa wa tamthilia. Tamthilia yake ya kuhuzunisha “Theluji katika Majira ya Joto” imechezwa kwa miaka 700 tokea ilipotungwa, na ilitafsiriwa kwa lugha nyingi na kuenea duniani.

Guan Hanqing aliishi katika karne ya 13, Enzi ya Yuan, alikuwa mtu mwerevu, mcheshi na mwenye elimu pana. Kadhalika, alikuwa hodari wa kupiga kinanda, kucheza ngoma, kupiga filimbi na kuwinda. Guan Hanqing kwa miaka mingi aliishi kwenye mji mkuu na aliwahi kuwa mganga katika hospitali ya kifalme, lakini alikuwa hana hamu na kazi hiyo bali alipenda zaidi kutunga tamthilia.

Katika miaka aliyoishi, jamii katika Enzi ya Yuan ilikuwa ya wasiwasi, na utawala ulikuwa mbaya, migongano kati ya matabaka na kati ya makabila ilikuwa mikubwa, wananchi waliishi vibaya. Guan Hanqing aliwahurumia sana watu maskini, aliacha wadhifa wake alikwenda miongoni mwa watu maskini ili kuwaelewa maisha yao na kwa kutumia tamthilia zake alifichua ubovu wa jamii na kuonesha matumaini yake.

Kutokana na kuwa alielewa sana maisha ya makabwera na kufahamu lugha zao, alipata uwezo mkubwa wa kuandika tamthilia zake. Tamthilia zake ziliwalilia watu walionyanyaswa na kuonesha moyo wa kupambana na unyanyasaji huo.

Tamthilia “Theluji katika Majira ya Joto” ilieleza uonevu uliompata msichana Dou E. Tamthilia hiyo ilipendwa sana na watazamaji katika karne kadhaa zilizopita, na inasifiwa kuwa ni moja ya tamthilia kumi za kuhuzunisha za China ya kale.

Maishani mwake Guan Hanqing aliandika tamthilia 67, lakini zilizobaki mpaka sasa ziko 18 tu. Katika tamthilia zake alikuwa makini sana kuumba taswira ya wahusika na kuonesha hisia za moyoni. Kati ya waandishi wa tamthilia hakuna hata mmoja kama yeye aliyefanikiwa kuumba sura nyingi mahususi zilizo tofauti katika tamthilia.

Guan Hanqing anachukua nafasi muhimu katika historia ya tamthilia na fasihi ya China, anasifiwa kama ni “Shakespeare wa Mashariki”.