Pu Songling na Riwaya Yake "Hadithi za Mashetani"
中国国际广播电台

      Mwanzoni mwa karne ya 18, kitabu maarufu cha hadithi fupi fupi yaani “Hadithi za Mashetani” kiliibuka nchini China, Pu Songling kwa ustadi wake aliandika hadithi nyingi za mashetani na bweha.

Pu Songling alizaliwa mwaka 1640 na kufa mwaka 1715, alikuwa mwanafasihi katika Enzi ya kifalme ya Qing. Alizaliwa katika ukoo wa wafanyabiashara, lakini alifanya kazi ya ualimu. Katika maisha yake aliandika makala mengi na kitabu chake cha mkusanyiko wa hadithi fupi yaani "Hadithi za Mashetani" ndicho kilichompatia umaarufu.

Kitabu cha “Hadithi za Mashetani” kimekuksanya hadithi 430, ambapo miongoni mwa hadithi hizo iliyo fupi kabisa ina maneno mia mbili au tatu hivi, na ile ndefu sana ina maelfu kadhaa ya maneno. Kitabu kizima kinaeleza hadithi za mashetani na bweha kikilaani pingu za maadili ya kimwinyi, ubovu wa mitihani ya kifalme ya kuchagua maofisa na kudai uhuru wa maisha ya binadamu. Katika kitabu hiki hadithi za kupendeza sana ni zile za mapenzi kati ya mashetani na bweha ambazo zilionesha matumaini ya binadamu kuvunja pingu za maadili ya kimwinyi kati ya wanaume na wanawake.

Katika kitabu cha “Hadithi za Mashetani” bweha hujitokeza kama kisura. Miongoni mwa hadithi hizo, maarufu zaidi ni “Hadithi ya Xiao Cui”. Hadithi hiyo iliandikwa kwa vituko vingi vya kuwavutia wasomaji, ambapo mwandishi alimsawiri kwa ustadi msichana mmoja mwenye akili, roho nzuri na wa kupendeza. Mwishoni mwa hadithi hiyo mwandishi alibainisha kwamba Xiao Cui alikuwa bweha mdogo, kwa sababu mama yake aliwahi kukimbia janga nyumbani kwa wale wazee, akajigeuza kuwa binadamu ili kuwalipa wema wao.

Katika kitabu cha "Hadithi za Mashetani", pia wako bweha wenye sura mbaya lakini roho nzuri. Hadithi ya “Bweha Mwenye Sura Mbaya” ilieleza jinsi bweha mmoja mwenye sura ya kuchukiza alivyomkuta msomi mmoja, ambaye alikuwa maskini hahehohe hata chakula kilikuwa ni shida kwake achilia mbali nguo. Bweha huyo alimsaidia maisha yake. Lakini baada ya msomi huyo kupata nguo safi, nyumba za fahari na kila kitu kwa maisha ya starehe alimwomba mchawi amfukuze bweha. Bweha alihamaki sana kutokana na msomi huyo kukosa shukrani, ndipo licha ya kurudisha yote aliyompa msomi, alimtuma shetani kumwadhibu vibaya. Kwa masimulizi ya hadithi hii mwandishi anawaonya watu wenye roho mbaya.

Katika kitabu cha "Hadithi za Mashetani" mwandishi Pu Songling pia alitunga hadithi ya bweha kisura lakini mwenye roho katili. Hadithi ya "Kuchora Ngozi ya Mrembo" ilieleza kuwa bweha mmoja alijifunika kwa ngozi yenye sura nzuri akiishi kwa kufyonza damu za binadamu, bweha huyo mwishowe aliuawa na binadamu.

Kwa kifupi, Pu Songling aliwaelezea wasichana wengi kwa sura ya bweha, na wasichana hao walikuwa na maadili mengi mazuri ambayo binadamu hawakuwa nayo.

"Hadithi za Mashetani" ni maandishi makubwa katika historia ya fasihi ya Kichina. Katika miaka mia mbili iliyopita hadithi hiyo imetafsiriwa kwa lugha zaidi ya 20, na hadithi nyingi zilitengenezwa kuwa filamu na michezo ya televisheni.