“ Mwanzo Dharau, Mwisho Heshima ”
中国国际广播电台


        “ Mwanzo Dharau, Mwisho Heshima ” ni msemo mmojawapo wa Kichina. Sasa nakusimulieni kisa chenyewe.

Karne ya tano kabla kuzaliwa Kristo ilikuwa Enzi ya Madola ya Kivita nchini China. Katika kipindi hiki yalikuwako madola mengi,lakini saba kati yao yaliyojitokeza zaidi, nayo ni Qin, Chu, Qi, Yan, Han, Zhao, Wei. Dola la Qin ambalo lilikuwa kaskazini-magharibi mwa China, yaani Jimbo la Shanxi kwa leo, lilikuwa na nguvu zaidi kwa sababu ya kufanya mageuzi ya kisiasa na kiuchumi. Dola hili lilikuwa mara nyingi likichokoza madola mengine sita. katika kukabiliwa na hali hiyo, ndani ya tawala za madola sita, yalitokea makundi mawili tofauti kuhusu namna ya kushughulikia Qin. Kundi moja lilitetea kwamba madola yote sita yafanye "yaungane na Qin", yawe marafiki na Qin na kujitahidi kutoudhi dola hilo isije ikawa kisingizio cha kuleta uchokozi. Kundi lingine lilitetea kwamba madola yote sita "yaungane dhidi ya Qin".

Walikuwako washauri wengi waliokuwa wakieneza utetezi wao katika madola yote saba. Iwapo utetezi fulani ungekubaliwa, mshauri mwenyewe angejulikana, thamani yake ingekuwa kubwa mno. Mshauri Su Qin alikuwa mmojawapo.

Mshauri huyo kwanza alifika katika Dola la Qin akijaribu kueneza utetezi wake wa "kuungana na Qin", kuhamasisha Dola la Qin kutuliza madola sita, na baadaye kuyateka. Qin ilikana utetezi wake kwa kusema kwamba haikuwa na hamu na utetezi huo, lakini ukweli ni kwamba wakati huo Dola la Qin lilikuwa bado halijatayarishwa vya kutosha kuyameza madola sita. Su Qin hakuwa na ujanja; ilikuwa karibu aishiwe na nauli na nguo zake zilikuwa zimechakaa, basi akarudi makwao kwa masikitiko.

Familia yake ilipomwona jinsi alivyokuwa katika simanzi, wazazi walikosa hamu ya kuzungumza naye; mkewe aliyekuwa akiendelea kufuma nguo hata hakumwinulia macho. Aliomba mke wa kaka yake ampatie chakula, lakini badala ya kuandaliwa chakula alilaumiwa. Su Qin aliona uchungu rohoni mwake, akaazimia kusoma ili kujiimarisha. Alikuwa akisoma usiku na mchana, kufafanua mbinu za kivita, usingizi ulipomwelemea aliweza hata kujichoma sindano kwenye paja lake. Na ndipo usemi wa "Kuchoma sindano ili kusoma" ukaanzia hapo.

Su Qin alifanya utafiti juu ya hali ya kila dola, mwishowe aliona kuwa "muungano dhidi ya Qin" ungeweza kukubalika, hivyo alianza kushawishi madola sita. Kweli muungano huo uliongozwa na Dola la Chu ukapatikana, Su Qin akawa kamanda mkuu. Kwa sababu ya muungano huo, Dola la Qin likatulia tuli lisithubutu kuvamia dola lingine. Utulivu huo uliendelea kwa miaka 15 mpaka mfalme Qin Shihuang alipounganisha China nzima.

Ilivyokuwa Su Qin alikuwa ni amirijeshi mkuu, amejipatia heshima kubwa katika madola sita. Siku moja alisafiri kikazi alipita nyumbani kwake Luo Yang. Kusikia habari hiyo maofisa wa sehemu waliamrisha kusafisha barabara, na walikuwa tayari mapema kumkaribisha foleni. Wazazi wake walisepetukasepetuka wakafika mwanzo wa njia wakimsubiri. Baada ya Su Qin alipofika nyumbani, mkewe alinyamaza pembeni asithubutu kutazamana naye uso kwa uso. Mke wa kaka yake ndiye aliyekuwa akinyenyekea kumsalimu. Su Qin alisema, "Shemeji, mbona unavyonifanyia leo ni tofauti kabisa na hali ya zamani. Kabla ya hapo ulinibeza, na sasa unanitukuza." Shemeji alijibu huku mwili ukimtetemeka, "Nawezaje kuthubutu kukutendea kama zamani, hali umekuwa mwenye cheo kikubwa na umetajirika sana." Su Qin alishusha pumzi na kusema, "Mtu akiwa maskini hudharauliwa na wazazi wake, akiwa tajiri hata jamaa zake humwogopa, hii ndio sababu ya watu kuyamezea mate madaraka!"

Hiki ndicho kisa cha msemo wa "Mwanzo dharau, mwisho heshima", ikieleza wale wanaopima watu kwa sura, au cheo na mali.