Yu Boya na Zhong Ziqi
中国国际广播电台


      
Katika kipindi cha Spring na Autumn, katika dola la Chu kulikuwa mwanamuziki mmoja ajulikanaye kwa jina la Yu Boya. Huyu Yu Boya alikuwa mwerevu toka alipokuwa mtoto, na alipenda sana muziki. Baadaye alijifunza kupiga kinanda kwa mwalimu wake Lian Cheng.

Baada ya kujifunza kwa miaka mitatu, alikuwa mwanamuziki mashuhuri, lakini Yu Boya hakuridhika, aliona kiwango chake kilikuwa bado si kikubwa kileleni. Mwalimu wake Lian Cheng alifahamu Yu Boya aliyofikiri moyoni, alimwambia kwamba atamwongoza kwa mwalimu wake ambaye ufahamu wake wa muziki ni wa juu sana. Yu Boya alikubali.

Baada ya kutayarisha chakula cha kutosha hao wawili walipanda mashua na kufika kwenye mlima wa Penglai. Mwalimu wake Lian Cheng alimwambaia, “Nisubiri hapa, nakwenda kumtafuta mwalimu wangu.” kisha akaondoka. Siku nyingi zilipita, lakini mwalimu wake Lian Cheng hakurudi. Boya aliangalia bahari isiyo na mwisho na misitu mlimani alihuzunika sana, kwa kusukumwa na moyo alipiga kinanda chake. Muziki ulijaa huzuni, lakini tokea hapo alikuwa mwanamuziki mkubwa. Kwa kweli mwalimu wake Lian Cheng alifanya hivyo kwa makusudi ili Yu Boya apate hisia za kweli moyoni.

Kuishi katika kisiwa kilichojitenga, usiku na mchana kitu alichoona ni bahari, ndege na misitu, siku nenda siku rudi hisia zake zilibadilika na kuelewa zaidi muziki, alitunga muziki maarufu uliowagusa mioyo wasikilizaji. Yu Boya alikuwa mwanamuziki mkubwa, lakini watu waliofahamu muziki wake walikuwa wachache.

Siku moja Yu Boya alisafiri kwa mashua, alipofika karibu na mlima, mvua kubwa ilinyesha, aliegesha mashua yake kukimbia mvua. sauti ya mvua na mandhari nzuri ya ukungu uliokuwa kwenye uso wa mto ilimsisimua, alipata msukumo wa kupiga kinanda. Muziki alioupiga ulikuwa ni sauti kutoka moyoni mwake. Kulikuwa na mtu mmoja kwenye ukingo wa mto akisikiliza muziki wake, mtu huyo aliitwa Zhong Ziqi.

Baada ya kusalimiana Yu Boya alimkaribisha Zhong Ziqi ndani ya mashua yake na kumpigia muziki. Zhong Ziqi alisikiliza kwa msisimko. Yu Boya alisema, “Katika dunia hii ni wewe tu unayefahamu sauti ya moyoni mwangu, wewe ndiye mwelewa sauti yangu!” Hao wawili walikuwa ndugu wa kuchanjiana.

Yu Boya aliahidiana na Zhong Ziqi kuwa watakutana baadaye. Siku moja Yu Boya alikwenda kwa Zhong Ziqi kama walivyoahidiana, lakini wakati huo Zhong Ziqi alikuwa amefariki. Baada ya kusikia habari hiyo Yu Boya alikimbilia kwenye kaburi la Zhong Ziqi na kumpigia muziki kwa huzuni kubwa, kisha alisimama na kuvunja kabisa kinanda chake. Tokea hapo Yu Boya aliacha kabisa kupiga kinanda.