Sun Wu
中国国际广播电台


      
Sun Wu aliyeishi katika karne ya sita K.K. ni mtu maarufu sana nchini na duniani, kitabu chake cha “Mbinu za Kivita za Sun Zi” kilikuwa ni maandishi makubwa ya kivita katika China ya kale.

Sun Wu alizaliwa mwaka 551 K.K. kilikuwa ni kipindi cha Spring na Autumn katika historia ya China. Alikuwa mtu wa dola la Qi, alipokuwa na umri wa miaka 19 alikwenda dola la Wu, na katika kiunga cha mji mkuu wa dola la Wu (mji wa Suzhou wa leo) aliandika kitabu chake cha mbinu za kivita na kumpa mfalme wa dola la Wu. Mfalme alifurahi sana, lakini hakujua kama mbinu zenyewe zinaweza kutumika, alimtaka Sun Wu afanye mazoezi kwa masuria waliokuwa ndani ya kasri la kifalme.

Sun Wu aliwagawa masuria 180 kwa vikundi viwili na kuwateua wawili waliopendwa sana na mfalme kuwa viongozi wa vikundi viwili, kimoja kulia na kingine kushoto, na kufanya mazoezi.

Sun Wu alisimama kwenye jukwaa na kuwafahamisha mpango wa mazoezi yake. Sun Wu alipiga ngoma ya kuanzisha mazoezi. Lakini masuria walikuwa kama hawajasikia mdundo wa ngoma, bali walichekacheka na kuchezacheza, safu zao zilivurugika, ingawa Sun Wu aliwaasa mara kadhaa, lakini haikusaidia kitu. Kutokana na hali hiyo, Sun Wu aliamuru kuwaua viongozi wawili.
Mfalme alipoona kweli Sun Wu alitaka kuwaua wapendwa wake wawili alimsihi awaache. Lakini Sun Wu hakubali ombi la mfalme, aliwaua. Kisha akaanza tena mazoezi, safari hii masuria walifanya mazoezi kwa makini, walipiga hatua mbele na nyuma, waliviringika na kutambaa kifudi fudi, kila mmoja alifanya vizuri. Kuona hali hiyo mfalme alifurahi, akamteua Sun Wu kuwa jemadari.

Chini ya uongozi wa Sun Wu jeshi la dola la Wu lilikuwa hodari sana na lilipata ushindi kila mara katika vita vya kupigana na madola mengine.

Mwaka 482 K.K. mfalme wa dola la Wu alikuwa mbabe kati ya madola yote kutokana na mbinu zilizoandaliwa na Sun Wu.

Kutokana na ushindi, mfalme alikuwa anavimba kichwa. Kwa kuona jinsi mfalme alivyokuwa, Sun Wu aliondoka na kuishi mbali na mfalme milimani.

Kitabu cha “Mbinu za Kivita za Sun Zi” ingawa kilikuwa na maneno elfu 6 katika makala 13, lakini kilionesha kikamilifu mbinu zake za kivita. Kitabu hicho kilisifiwa na watu wa baadaye kuwa ni “kitabu cha kwanza duniani kuhusu mbinu za kivita”, na kilitumika sana katika mambo ya kijeshi, kisiasa na uchumi.