Sera ya Dini ya China

Radio China Kimataifa

Baada ya kuzaliwa kwa China mpya mwaka 1949, serikali ya China imetunga na kutekeleza sera ya uhuru wa kuamini dini, na kuanzisha uhusiano kati ya mambo ya siasa na dini unaoambatana na hali halisi ya mazingira ya China. Raia wa China wana uhuru wa kuchagua imani yao ya kidini na kutangaza utambulisho wao wa kidini. Dini mbalimbali zina hadhi sawa, na kuwepo kwa pamoja, hakuna migogoro ya kidini nchini China. Waumini wa dini wanaheshimiana na wasioamini dini, na wanaishi vizuri kwa pamoja.

Katiba ya Jamhuri ya watu wa China inaeleza kuwa, wakazi wa Jamhuri ya Watu wa China wana uhuru wa kuamini dini. Idara yoyote ya kitaifa, jumuiya yoyote ya kijamii au mtu yeyote hana haki ya kuwalazimisha watu wengine kuamini au kutoamini dini fulani. Nchi inahakikisha shughuli za kawaida za kidini. Mtu yeyote haruhusiwi kutumia dini kufanya shughuli za kuharibu utaratibu wa kijamii, kudhuru afya ya wakazi wengine na kuzuia utekelezaji wa utaratibu wa elimu wa taifa. Jumuiya ya kidini na shughuli za kidini haziwezi kudhibitiwa na nguvu yoyote kutoka nchi za nje.

Sheria ya Kujiendesha Katika Maeneo ya Makabila Madogo, Kanuni ya Sheria ya Raia, Sheria ya Elimu, Sheria ya Kazi, Sheria ya Elimu ya Lazima, Sheria ya Uchaguzi wa Bunge la Umma, Sheria ya Uundaji wa Kamati ya Wanavijiji na Sheria ya Matangazo nchini China pia zinaeleza kuwa: wakazi wana haki ya kuchagua na kuchaguliwa bila kujali dini zao; mali halali za makundi ya kidini zinalindwa kisheria; elimu na shuguli za dini vimetenganishwa, wakazi wana haki sawa ya kupata elimu bila kujali uamini wao ya dini; watu wa makabila tofauti wanatakiwa kuheshimiana katika lugha na maandishi, mila na desturi na dini tofauti; wakazi hawawezi kubaguliwa kutokana na dini yao katika kutafuta kazi; matangazo na chapa za bidhaa haziruhusiwi kuwa na mambo yenye ubaguzi wa kikabila na kidini.

Mwezi Januari mwaka 1994, serikali ya China ilitangaza utaratibu wa usimamizi wa mahali pa kufanyia shughuli za kidini, ili kulinda haki na maslahi halali ya kutumia sehemu fulani kwa ajili ya shughuli za kidini. Mwezi Februari mwaka huo, serikali ya China pia ilitangaza utaratibu wa usimamizi wa shughuli za dini za wageni nchini Jamhuri ya Watu wa China, kuheshimu uhuru wa wageni waishio nchini China wa kuamini dini, na kuhakikisha mawasiliano ya kirafiki na maingiliano ya taaluma za utamaduni kati ya wageni na watu wa fani ya kidini nchini China.

Sheria husika za China zinaeleza kuwa: shughuli za kawaida za wafanyakazi wa dini, shughuli za kawaida za kidini zinazofanywa kwenye sehemu za kufanyia shughuli za kidini au nyumbani kwa waumini wa dini zinadhibitiwa na jumuiya za kidini au waumini wa dini wenyewe, zinalindwa kisheria, mtu yeyote haruhusiwi kuingilia kati shughuli hizo.

Kama ilivyo kwa nchi nyingi duniani, China pia inafuata kanuni ya kutenganisha shughuli za dini na elimu, na kutotoa elimu ya kidini kwa wanafunzi wa kawaida. Baadhi ya vyuo vikuu na taasisi za utafiti zinafanya utafiti na kutoa mafunzo maalum ya kidini. Katika vyuo vya kidini vilivyoendeshwa na jumuiya za dini mbalimbali, zinatoa elimu ya kozi maalum ya kidini kutokana na mahitaji yao.

Katika historia ndefu, utamaduni wa kidini umekuwa sehemu moja ya utamaduni wa jadi wa China. Dini zote zinatetea kuhudumia jamii, na kuleta baraka kwa wananchi.