Majengo ya Kasri

中国国际广播电台

      
Majengo ya kasri kwa maneno mengine ni majengo ya kifalme. Ni majengo yanayojengwa kwa ajili ya kuimarisha utawala wa wafalme, kutukuza heshima na mamlaka ya wafalme, kukidhi maisha yao ya anasa kiroho na kimali. Kwa hiyo majengo hayo yote yana lengo la kuonesha ufahari.


 

Kuanzia Enzi ya Qin (221-206 K.K.) nchini China “kasri” lilikuwa ni makazi ya wafalme na jamaa wa wafalme, na ni mahali pa wafalme kushughulikia mambo ya taifa. Ukubwa wa majengo ya kasri uliongezeka kutoka enzi hadi enzi, tofauti yake na majengo mengine ni paa la vigae vyenye rangi ya dhahabu, michoro ya rangi kwenye boriti, ngazi za marumaru, na majengo mengine pembeni mwa kasri. Kasri la Kifalme mjini Beijing ni kielelezo kizuri cha majengo hayo.         

      Ili kutukuza madaraka ya kifalme na kuonesha kiini cha utawala, majengo ya kifalme yalikuwa yakijengwa kwa ulinganifu kwenye pande mbili za mstari, majengo yaliyojengwa kwenye mstari wa katikati ni makubwa na ya kifahari, na majengo yaliyokuwa kwenye pande mbili za mstari wa katikati ni mafupi na ya kawaida. Kutokana na maadili ya kijamii nchini China ikiwa ni pamoja na kuheshimu mababu, heshima kwa wazee na kuabudu miungu ya ardhi, mbele ya kasri kwenye upande wa kushoto kunajengwa hekalu la kufanyia tambiko kwa mababu, na upande wa kulia hujengwa hekalu la kufanyia tambiko kwa miungu ya ardhini na nafaka. Mpangilio huo unaitwa “mababu upande wa kushoto na miungu upande wa kulia”. Na majengo yaliyopo kwenye mstari wa katikati pia yanagawanyika katika sehemu mbili, yaani sehemu ya mbele ni mahali pa kushughulikia mambo ya utawala, na sehemu ya nyuma ni makazi ya wafalme na masuria.