Majengo ya Mahekalu

中国国际广播电台

      

Mahekalu ni moja ya aina ya majengo ya dini ya Buddha nchini China. Mahekalu nchini China yalianzia India, mahekalu hayo ni ishara ya hali ya ustawi wa dini ya Buddha katika historia, ni majengo yenye thamani kubwa kwa ajili ya uchunguzi na usanii.

Wahenga wa China walizingatia sana ulinganifu wa majengo kwenye kando mbili za mstari wa katikati, hali kadhalika kwenye ujenzi wa mahekalu ya dini ya Buddha. Lakini pia kuna mahekalu yaliyojengwa kama bustani. Aina hizo mbili zinayafanya mahekalu nchini China yawe na taadhima na uzuri wa kimaumbile.

Mpangilio wa ujenzi wa hekalu la kale ni kuwa mbele kuna lango, na baada ya kuingia kwenye lango hilo upande wa kushoto na kulia kuna jumba la kengele na jumba la ngoma, na nyumba kubwa inayokabili lango ni ukumbi wa mungu, ndani ya ukumbi huo kuna sanamu za walinzi wanne wa peponi, nyuma ya ukumbi huo na kuendelea ni ukumbi wa mwasisi wa dini ya Buddha, Sakyamuni. Ukumbi huo ni mkubwa na ni muhimu kabisa kuliko majengo yote ndani ya hekalu. Mahekalu yaliyojengwa kabla ya enzi za Sui (581-618) na Tang (618-907) kwa kawaida hujengwa pagoda mbele ya hekalu au katikati ya ua wa hekalu, na baada ya enzi za Sui na Tang nafasi ya jengo la pagoda imechukuliwa na ukumbi mkubwa, na pagoda hujengwa katika ua mwingine.

 

Hekalu la Baimasi
Hekalu hili liko katika mji wa Luoyang mkoani Henan, lilijengwa katika Enzi ya Han (206-220 KK.). Hilo ni hekalu la mwanzo kabisa kati ya mahekalu ya dini ya Buddha yaliyojengwa na serikali nchini China. Ujenzi wake ni wa umbo la mstatili kwenye eneo la mita za mraba elfu 40. Ujenzi wa hekalu hilo ulichangia ustawi wa dini ya Buddha nchini China na hata nchi za Asia ya Mashariki na ya Kusini. Hadi sasa hekalu hilo linaendelea kuwa mahali patakatifu kwa waumini wa dini ya Buddha wa nchi nyingi.

Mahekalu katika Mlima Wutaishan
Mlima Wutaishan ni sehemu maarufu ya dini ya Buddha, kuna majengo 58 ya dini ya Buddha mlimani, na kati ya majengo hayo kuna mahekalu ya Nanchansi na Foguangsi yaliyojengwa katika Enzi ya Tang. Hekalu la Nanchansi ni hekalu lenye miaka mingi zaidi kati ya mahekalu yaliyojengwa kwa mbao nchini China. Hekalu hilo lina sifa zote za mahekalu ya enzi mbalimbali nchini China. Kutokana na uhodari wa ujenzi wake, sanamu, picha za ukutani na maandishi ya brashi ya wino, vinasifiwa kuwa ni “maajabu manne”.
 

Hekalu la Xuankongsi
Hekalu hili lastahili kutajwa, kwani ni jengo la ajabu lililojengwa kwenye genge kali mlimani. Hekalu hilo liko umbali wa km. 3.5 kutoka mji mkuu wa wilaya ya Hunyuan, ni jengo lililojengwa kwa mbao. Hekalu hilo lilijengwa katika Enzi ya Wei Kaskazini (386-534), na liliwahi kukarabatiwa katika enzi za Tang, Jin, Ming na Qing. Hekalu hili linakabiliana na mlima Hengshan, na hakuna madaraja ya kupandia, mandhari yake ni ya ajabu katika mlima Hengshan.

Kasri la Potala
Madhehebu ya Lama ni moja ya madhehebu ya dini ya Buddha nchini China, mahekalu ya Lama hujengwa kwa ukumbi mkuu na ukumbi wa kuombea dua. Mahekalu ya madhehebu ya Lama hujengwa mbele ya mlima. Kasri la Potala lililoko mkoani Tibet ni hekalu la madhehebu ya Lama, lilijengwa katika Enzi ya Tang (618-907), na baada ya enzi nyingi kukarabati na kupanua kasri hilo limekuwa na majengo mengi. Kasri hilo lina eneo la mita za mraba elfu 20, kuna kumbi kubwa zaidi ya 20, ndani ya ukumbi mkubwa wa mbele iliwekwa sanamu ya shaba ya mwasisi wa dini ya Buddha, Sakyamuni, iliyopakwa rangi ya dhahabu kwa kulingana sawa na mwili wake alipokuwa na umri wa miaka 12. Kasri la Potala ni jengo lenye mtindo halisi wa ujenzi wa Enzi ya Tang na pia limechukua mitindo ya India na Nepal.