Shirika la Umoja wa Mataifa lalaani shambulizi dhidi ya msafara wa msaada nchini Sudan Kusini
2021-09-23 08:39:24| CRI

Shirika la misaada ya kibinadamu la Umoja wa Mataifa limelaani vikali shambulizi la hivi karibuni dhidi ya msafara wa misaada huko Yei katika jimbo la Kati la Ikweta nchini Sudan Kusini, eneo ambalo katika siku za nyuma lilikuwa limeathriwa na mashambulizi dhidi ya magari ya kiraia.

Kaimu mratibu wa misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini Bw. Matthew Hollingworth, ametoa wito kwa mamlaka na jamii kuhakikisha usalama wa wafanyakazi wa kibinadamu wanaotoa misaada ya kuokoa maisha ya watu walio katika mazingira magumu.

Bw. Hollingworth amesema Septemba 17, msafara wa mshirika anayeshirikiana na Shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa WFP, uliokuwa na watu saba katika malori matatu, ulishambuliwa katika mji wa Mugwo Payam, Kaunti ya Yei, ukiwa na tani 121 za chakula zilizokusudiwa kwa ajili ya watu katika kaunti ya Morobo. Dereva wa lori moja raia wa Sudani Kusini, na watu wengine walijeruhiwa.