Umoja wa Mataifa umetoa dola milioni 25 za Kimarekani kama msaada wa haraka kwa watu walioathiriwa zaidi na ukame nchini Somalia.
Mratibu wa Umoja huo anayeshughulikia masuala ya kibinadamu nchini Somalia Adam Abdelmoula, amesema fedha hizo ni muhimu katika kuzuia mateso zaidi na kuokoa maisha. Ameongeza kuwa zaidi ya watu milioni 4.3 nchini Somalia wameathiriwa na ukame, kati yao zaidi ya nusu milioni wamekimbia makazi yao, na idadi hiyo bado inaongezeka.
Amesema msaada huo utapelekwa kwenye maeneo ambayo hayajahudumiwa vizuri na ni vigumu kufikiwa, wakati maafa ya ukame yameongeza umaskini na kuhatarisha maisha huko.