Mawaziri wa China na Russia wazungumzia mgogoro wa Ukraine
2023-03-03 09:53:09| CRI

Waziri wa Mambo ya Nje wa China Bw. Qin Gang amekutana na mwenzake wa Russia Bw. Sergei Lavrov na kuzungumza kuhusu uhusiano wa nchi hizo mbili na utatuzi wa kisiasa wa mgogoro wa Ukraine, pembeni ya Mkutano wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Kundi la nchi 20 (G20) uliofanyika New Delhi, India.

Bw. Qin amesema chini ya mwongozo wa kimkakati wa marais wa nchi hizo mbili, uhusiano kati ya China na Russia umedumisha maendeleo thabiti, na kuweka mtazamo mpya kwa aina mpya ya uhusiano kati ya nchi kubwa, pamoja na kubeba jukumu muhimu katika kukuza mshikamano na ushirikiano kati ya masoko yanayoibukia na nchi zinazoendelea. Nchi hizo mbili zinapaswa kudumisha mawasiliano katika ngazi zote na kuongeza mawasiliano na uratibu kati ya wizara zao za mambo ya nje.

Kwa upande wake, Lavrov amesema yuko tayari kushirikiana na China katika kutekeleza makubaliano yaliyofikiwa na wakuu wa nchi hizo mbili, kuzidisha mawasiliano ya hali ya juu na kupanga ushirikiano katika nyanja mbalimbali.