• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • China yatangaza hatua nne za kufungua zaidi mlango wake kwa nje

    (GMT+08:00) 2018-04-10 19:04:48

    Leo asubuhi, mkutano wa mwaka wa 2018 wa Baraza la Asia la Boao umefunguliwa huko Boao, mkoani Hainan, China. Rais Xi Jinping wa China ametoa hotuba akitangaza hatua nne muhimu zinazolenga kuimarisha ufunguaji mlango wa China kwa nje zaidi.

    Katika hotuba yake, rais Xi Jinping wa China amesema mlango wa China utazidi kufunguliwa na kuahidi kuwa China itapanua kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa soko, kutengeneza mazingira ya uwekezaji yanayovutia zaidi, kuongeza nguvu ya kulinda hakimiliki za ubunifu na kuongeza kuagiza bidhaa kutoka nje.

    Anasema, "China itaimarisha kuungana na kanuni za kiuchumi na kibiashara za kimataifa, kuongeza uwazi, kuongeza nguvu za kulinda hakimiliki, kushikilia utawala wa sheria, kuhamasisha ushindani na kupambana na ukitirimba. Katika miezi sita ya kwanza ya mwaka huu, tutakamilisha marekebisho ya orodha hasi kwenye uwekezaji wa kigeni na kutekeleza mfumo wa usimamizi ulio kwenye msingi wa mitaji ya kigeni kutendewa kama mitaji ya ndani pamoja na orodha hasi. Mwaka huu tutaifanyia mabadiliko Ofisi ya Hakimiliki ya Ubunifu ya Taifa, kukamilisha utekelezaji wa sheria, kuongeza kwa kiasi kikubwa adhabu ya kukiuka sheria na kuonesha vya kutosha ufanisi wa sheria husika."

    Vilevile rais Xi Jinping amesema China itahamasisha mawasiliano ya kiteknolojia ya kawaida na ushirikiano kati ya makampuni ya kichina na kigeni na kulinda hakimiliki za ubunifu za makampuni ya kigeni.

    Akizungumzia hatua hizo mpya za China, mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa IMF Bibi Christine Lagarde anasema, "Katika hotuba yake, rais Xi Jinping ameahidi kufungua mlango zaidi kwenye mambo ya fedha, bima na magari, kupunguza vizuizi vya kibiashara, kuweka mazingira yenye usawa ya kibiashara, na kulinda hakimiliki. Kama hatua hizo kabambe zitatekelezwa, inaaminika kuwa China itapata mafanikio zaidi katika miaka 40 ijayo, mbali na mafanikio ya mageuzi na ufunguaji mlango iliyopata katika miaka 40 iliyopita."

    Naye ofisa mkuu mtendaji wa kampuni ya FMG ya Australia Elizabeth Gaines amesema kwa makampuni ya kigeni, kufungua zaidi soko la China kunamaanisha fursa nyingi zaidi za maendeleo. Anasema,"Naona mageuzi na ufunguaji mlango vimeingia kwenye kipindi kipya, na katika hotuba yake, rais Xi Jinping amesema kuwa China itahamasisha uwekezaji, kufungua soko la mambo ya fedha na bima, kuongeza kuagiza bidhaa kutoka nje. Naona hii ni hotuba ya kuchangamsha, na kuonesha ishara kuwa China itatekeleza mageuzi na ufunguaji mlango kwa muda mrefu."

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako