• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Uchunguzi kuhusu uingiliaji wa Russia kwenye uchaguzi wa Marekani huenda utasababisha pigo kubwa rais Trump

    (GMT+08:00) 2018-08-07 17:07:33

    Jumapili iliyopita rais Donald Trump wa Marekani alisema kupitia ukurasa wake wa Twitter kuwa ripoti kuhusu mtoto wake Donald Trump Jr. zote ni "habari feki", na pia amekiri kuwa mwaka 2016 mtoto wake huyo alikutana na mwanasheria wa Russia kwa ajili ya kupata taarifa za kiintelijinsia kuhusu mpinzani wake wa kisiasa, na kukitaja kitendo hicho kuwa ni "halali kikamilifu na ni mazoea ya kawaida kwenye duru za kisiasa".

    Zaidi ya mwaka mmoja uliopita, wakati gazeti la New York Times lilipofichua mkutano huo, Bw. Donald Trump Jr. alitoa taarifa kuwa walijadiliana kuhusu mradi uliositishwa wa serikali ya Marekani wa kuasili watoto wa Russia, na kuhakikisha kuwa baba yake rais Trump hakujua kuhusu mkutano huo. Lakini miezi michache baadaye vyombo vya habari vilifichua kwamba taarifa hiyo ilitungwa chini ya idhini ya rais Trump mwenyewe.

    Vyombo vikubwa vya habari vya Marekani na Ulaya vimesema mkutano huo wa mwaka 2016 ulikuwa ni jambo muhimu lililopewa kipaumbele kwenye uchunguzi kuhusu uingiliaji wa Russia katika uchaguzi mkuu wa Marekani. Wakati uchaguzi wa kipindi cha kati wa Marekani unapokaribia, vyombo vikubwa vya habari vya Marekani ikiwemo Washington Post, CNN na AP, vyote vilitoa ripoti Jumapili kuwa uchunguzi huo huenda utawaathiri watu wa karibu wa rais Trump, haswa mtoto wake mkubwa Donald Trump Jr.

    Wataalamu wa sheria wanaona Bw. Donald Trump Jr. kukutana na mgeni kwa ajili ya kupata taarifa za kiintelijinsia kuhusu mpinzani wake wa kisiasa, kumekiuka vipengele husika vya sheria ya uchaguzi ya Marekani, na hata anaweza kukabiliwa na tuhuma za kufanya njama dhidi ya Marekani. Mwanzoni mwa mwaka huu, mshauri mkuu wa mikakati wa Ikulu ya Marekani Bw. Steve Bannon alipoondoka kutoka kwa rais Trump, aliutaja wazi mkutano huo kama "kitendo cha kihaini".

    Kabla ya hapo, mhusika mwingine muhimu wa mkutano huo ambaye alikuwa ni meneja wa kampeni ya rais Trump Bw. Paul Manafort, amekabiliwa na mashtaka mengi ikiwemo kufanya njama dhidi ya Marekani, na hivi sasa yuko kizuizini na kusubiri kusikilizwa kesi yake mwezi ujao. Hata hivyo habari zinasema Bw. Paul Manafort hajakiri makosa yake. Kama akikiri mashtaka, Bw. Manafort atakuwa shahidi muhimu kwenye uchunguzi kuhusu uingiliaji wa Russia katika uchaguzi wa Marekani wa mwaka 2016.

    Kabla ya kesi ya Bw. Manafort kusikilizwa mahakamani, rais Trump alijaribu kumtetea kupitia ukurasa wake wa Twitter, na kusema uchunguzi huo hauna ushahidi wowote, na kumwagiza waziri wa sheria Bw. Jeff Sessions kusitisha mara moja uchunguzi huo.

    Hivi sasa uchunguzi huo umekaribia kumalizika, rais Trump anakabiliwa na machaguo magumu, kukubali kuhojiwa na mchunguzi maalumu Bw. Robert Mueller, au kumsubiri kuitwa na Bw. Mueller kujibu maswali. Safari hii haijulikani rais Trump atazusha jambo gani duniani, ili kugeuza ufuatiliaji wa umma kuhusu yeye.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako